Dar es Salaam. Mfanyabiashara Zakayo Tundulilo amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akikabiliwa na mashtaka matatu likiwemo la kutakatisha Sh1.2 milioni.
Tundulilo maarufu kama Gambo ambaye ni mfanyabiashara alitajwa na Mkurugenzi wa Mashtaka Tanzania ( DPP), Biswalo Mganga kuwa anajihusisha na vitendo vya rushwa.
Mganga amesema mshtakiwa hiyo alitoa gerezani hivi karibuni baada ya kuingia makubaliano ya kukiri makosa na ofisi ya DPP, lakini baada ya kutoka inadaiwa alifanya udanganyifu kwa kuwatapeli watu kuwa wakimpa fedha, atawasaidia nao waweze kujadiliana na ofisi hiyo mapema,.
Mganga amesema mtuhumiwa huyo anadaiwa kuzunguka kuchukua fedha kwa ndugu wenye kesi za uhujumu uchumi na kuwaambia kuwa atawapeleka kwenye ofisi ya DPP ili awaze kuwasaidia ndugu zao watoke mapema kwa utaratibu wa majadiliano na DPP, jambo ambalo ni kinyume cha sheria.
Mshtakiwa huyo amesomewa mashtaka yake leo Jumatano Machi 12, 2020 na wakili wa Serikali mwandamizi, Wankyo Simon mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi, Rashid Chaungu.
Simon amedai kuwa mshtakiwa huyo anakabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi namba 21/2020.
Pia Soma
- Tanzania yapongezwa kudhibiti dawa za kulevya
- Waziri Ikupa awafunda wanawake walemavu
- Tanzania kuadhimisha wiki ya maji bila wageni kutoka nje, corona yatajwa
- VIDEO: Mchungaji Msigwa atoka jela
Mshtakiwa huyo anadaiwa kuchukua fedha kwa ndugu wa Ntalima, ambaye ni Emmanuel Ntalima ili amsaidie ndugu yake ambaye ana kesi ya uhujumu uchumi namba 7/2019 iliyopo mahakamani hapo afanye makubaliano mapema na DPP.
Shtaka la pili, siku na eneo hilo mshtakiwa alijihusisha na vitendo vya rushwa kwa kuahidi kiasi hicho anakipeleka ofisi hizo ili wamsaidie ndugu aweze kufanya mchakato wa kutoka haraka.
Katika shtaka la tatu ambalo ni utakatishaji fedha, wakili Simoni amedai siku hiyo mshtakiwa huyo alijipatia fedha hizo huku akijua ni kosa tangulizi la kujihusisha na vitendo vya rushwa.
Mshtakiwa baada ya kusomewa mashtaka yake, hakutakiwa kujibu chochote kutokana na shtaka la utakatishaji fedha kutokuwa na dhamana kisheria.
Upande wa mashtaka ulidai kuwa upelelezi haujakamilika na kuomba tarehe nyingine kwa ajili ya kutajwa.
Hakimu Chaungu ameahirisha kesi hiyo hadi Machi 24, 2020 itakapotajwa tena na kurudishwa rumande kutokana na mashtaka yanayomkabili kutokuwa na dhamana.