Dar es Salaam. Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam nchini Tanzania linamshikilia Khamis Luwonga maarufu Meshack mkazi wa Kigamboni kwa tuhuma za kumuua mkewe, Naomi Marijani.
Luwonga anadaiwa aliuchoma moto mwili wa mkewe.
Mkuu wa Upepelezi wa kanda hiyo, Camillius Wambura akizungumza na Mwananchi leo Jumatano Julai 17, 2019 amesema wanamshikilia kwa mahojiano kuhusu tukio hilo.
Amesema pamoja na kumhoji polisi wamekwenda katika maeneo ambayo ameyataja kufanya mauaji hayo kwa ajili ya kupata uthibitisho.
“Huyu bwana tunaye tunaendelea kumhoji na askari wameshakwenda katika maeneo aliyoyataja, wamechukua majivu kwa ajili ya vipimo vya DNA kuona kama kweli yanaendana na huyo mama,” amesema
Joseph Hatia, shemeji yake Naomi amedai kumekuwa na taarifa kuwa Naomi na mumewe hawakuwa na maelewano mazuri hadi siku anatoweka.
Pia Soma
- Umahiri wa Faru Rajabu unavyoleta matumaini ya kuongeza idadi yao Tanzania
- UBISHI MPYA; Zari na mama Diamond nani mkubwa?
“Wakiwa wanagombana na kusukumana amedai kwamba Naomi alidondoka na kujigonga kichwani, alivyoona hivyo akamburuza hadi nje na kuchimba shimo akamtumbukiza na kuchoma moto.”
Hatia amesema kwa sasa familia inasubiri taarifa rasmi kutoka kwa polisi ambao wanaendelea kumshikilia Luwonga.
Naomi alitoweka nyumbani kwake Mei 15, 2019 na familia yake ilitoa taarifa polisi katika kituo cha Chang’ombe baada ya mumewe kuwajulisha siku nne tangu atoweke.