Dar es Salaam. Mfanyabiashara Mohamed Kiluwa (50) amekutwa na kesi ya kujibu katika mahakama ya Wilaya ya Ilala na ataanza kujitetea Desemba 17, 2018.
Uamuzi huo umetolewa leo Jumanne Desemba 11, 2018 na hakimu mkazi, Samuel Obasi baada ya upande wa mashtaka kufunga ushahidi wao.
Kiluwa anakabiliwa na shtaka moja la kutoa rushwa ya Dola za kimarekani 40,000 kwa Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi.
Akisoma Uamuzi huo baada ya upande wa mashtaka kufunga ushahidi wao leo, Hakimu Obasi amesema "Upande wa mashtaka ulileta mashahidi sita pamoja na vielelezo vingi ikiwemo hati za Ardhi na CD.”
Hakimu Obasi amesema amepitia ushahidi wa mashahidi hao pamoja na vielelezo na kumuona mshtakiwa kuwa ana kesi ya kujibu.
“Baada ya kupitia ushahidi na vielelezo hivi, mahakama yangu imemkuta Kiluwa ana kesi ya kujibu, hivyo chini ya kifungu namba 231(1) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai, mshtakiwa anatakiwa kujitetea,” amesema Obasi.
Baada ya kueleza hayo wakili wa mshtakiwa, Omary Madega amedai upande wa utetezi watakuwa na mashahidi wawili, akiwemo Kiluwa.
Awali, kabla ya hakimu kutoa uamuzi huo upande wa mashtaka walikuwa na shahidi moja ambaye alitoa ushahidi wake dhidi ya Kiluwa.
Shahidi huyo, Wilson Luge (39) ambaye ni Kaimu Kamishna wa Ardhi Msaidizi wa Wizara ya Ardhi, amedai kuwa yeye ndio aliyeshiriki zoezi la kuhakiki na kuhesabu fedha hizo Dola za 40,000 za Marekani ambazo zilikuwa katika bahasha ya kaki, juu ya meza ya waziri Lukuvi.
Akiongozwa na mawakili kutoka Takukuru, Maghela Ndimbo akisaidiana na Nikson Shayo, Luge ambaye ni shahidi wa sita katika kesi hiyo, amedai kuwa baada ya kuzihesabu fedha hizo walizianisha katika fomu maalum na kisha kuisaini fomu hiyo kama sheria inavyotaka.
Hakimu Obasi ameahirisha kesi hiyo hadi Desemba 17,2018 itakapoendelea kwa upande wa utetezi kuanza kujitetea.
Tayari mashahidi sita wa upande wa mashtaka wameshatoa ushahidi dhidi ya Kiluwa, akiwemo Waziri Lukuvi.
Katika ushahidi wake Lukuvi amedai kuwa alipigiwa simu na msiri wake kuwa kuna fedha chafu kiasi cha dola 40,000milioni za Marekani zinaletwa ofisini kwake.
Amedai fedha hizo zinapelekwa na Kiluwa ambaye ni Mkurugenzi wa Kampuni ya Kiluwa Steal Group and Co. Ltd na Kiluwa Free Processing Zone.
Aliieleza mahakama kuwa anatambua kuna mradi wa uwekezaji kwa ajili ya ujenzi wa viwanda uliopo eneo la Mlandizi , wilayani Kibaha.
Lukuvi amedai kuwa eneo hilo lina ukubwa wa ekari 1000 na kwamba mmoja wa wamiliki wa mradi huo ni mshtakiwa Kiluwa.
Amedai mshtakiwa aliomba kupimiwa viwanja 73 na kwamba Juni na Julai, 2018 alikuwa amepatiwa hati ya viwanja 57 huku vikibaki viwanja 16 ambavyo vilikuwa havijatolewa hati na msajili.
Alieleza kabla ya kumpa hati hizo 57, Lukuvi alitoa masharti kwa mshtakiwa huyo, kuwa viwanja hivyo viendelezwe ndani ya miaka miwili na asipofanya hivyo atanyang’anywa viwanja kwa mujibu wa sheria.
Lukuvu amedai mbali na kutoa masharti kwa Kiluwa, pia alitoa maelekezo kwa msaidizi wake ambaye ni Kamishana wa Ardhi wa Kanda ya Dar es Salaam, Mathew Nhonge kuwepo na masharti ya kuendeleza eneo hilo ndani ya miaka miwili.
Hata hivyo, Lukuvi amedai kuwa Mathew hakuweka masharti katika hati hizo hali liliyosababisha Lukuvi kumtaka Kiluwa kuwasilisha hati hizo ofisini kwake ili azikague.
Katika kesi ya msingi, Kiluwa anakabiliwa na shtaka moja la kutoa rushwa kwa Waziri Lukuvi.
Inadaiwa kuwa Julai 16, 2018 katika ofisi za waziri huyo zilizopo Magogoni, Kiluwa alitoa rushwa ya Dola 40,000 za Marekani ( Sh90 milioni).
Inadaiwa kuwa mshtakiwa huyo alitoa fedha hizo ili asiwasilishe hati ya umiliki wa viwanja 57 vilivyopo Kitalu B Kikongo na Kitalu D Disunyara katika eneo la viwandani, Kibaha mkoani Pwani.
Soma Zaidi: Mahakama yasikiliza CD kesi ya Lukuvi