Dar es Salaam. Kijana Shabani Hamisi amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kinondoni akikabiliwa na kosa la kumtishia silaha aina ya bastola, Venance John.
Kufikishwa kwa mshtakiwa huyo imepita siku tatu tangu Inspekta Jenerali wa Polisi nchini Tanzania (IGP), Simon Sirro kumtaka kijana aliyemtishia mwenzake bastola kuripoti polisi baada ya kuonekana akifanya kitendo hicho katika picha za video zinazosambaa katika mitandao mbalimbali ya kijamii nchini.
Akisoma hati ya mashtaka mbele ya Hakimu Mfawidhi, Frenk Moshi, Wakili wa Serikali Mwandamizi, Mkunde Mshanga amedai kuwa mshtakiwa huyo anakabiliwa na shtaka la kutishia kwa kutumia nguvu.
Mshanga ameeleza kuwa Oktoba 30 , 2019 maeneo ya mbezi Mabwepande mshtakiwa huyo alikutwa na bastola yenye namba ya usajili 102969 kwa makusudi alimtishia Venance huku akijua kufanya hivyo ni kosa la kisheria .
Baada ya kusomewa shtaka hilo mshtakiwa alikana ambapo upande wa mashtaka ulidai kuwa hauna pingamizi na dhamana.
Hakimu Moshi amesema dhamana ipo wazi kinachotakiwa mshtakiwa awe na wadhamini wawili ambao wanatakiwa wafanyakazi au wakulima kila mmoja atasaini bondi ya Sh2 milioni.