Serengeti. Marwa Maduka, mkazi wa Rung’abure Wilaya ya Serengeti aliyetoroka baada ya kudaiwa kumkata mkewe kwa chupa kutokana na wivu wa mapenzi amekamatwa akifanya kibarua katika mgodi wa dhahabu.
Akizungumza na Mwananchi leo Februari 13, 2020 mkuu wa Wilaya ya Serengeti, Nurdin Babu amesema Maduka alikamatwa Februari 11, 2020 katika mgodi mdogo wa dhahabu ulioko kijiji cha Merenga.
Maduka alitoroka Februari 3, 2020 baada ya kumpiga kisha kumkata kwa chupa usoni mkewe, Esther Makenge (19) kwa madai wa kuchelewa kurudi nyumbani akitoka kwenye biashara zake.
Mwenyekiti wa Serikali ya kijiji cha Merenga, Moses Ryoba amesema kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo kumetokana na baadhi ya wachimbaji mgodini hapo kumtambua, kutoa taarifa kituo kidogo cha polisi Machochwe.
Akizungumza na Mwananchi akiwa hospitalini, Esther amesema mumewe alimtuhumu kuwa alichelewa kurudi nyumbani kwa sababu alikuwa na wanaume wengine.
“Baada ya kunipiga ngumi na mateke, alichukua chupa ya bia akanipiga nayo na ilipopasuka akaanza kutumia kipande kunikata usoni,” amesema Esther.
Pia Soma
- TANZIA: Nsa Kaisi afariki dunia
- Mwili wa Idd Simba kuzikwa kesho
- Tasaf waja na mpango mwingine kusaidia kaya masikini
- Watoto 6,927 nchini Tanzania watoa taarifa ukatili wa kijinsia