Juma Hamad Saleh (19) mkazi wa Msuka Konde amekamatwa akidaiwa kuwa na bangi katika kituo cha kupigia kura Jimbo la Konde.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kaskazini Pemba, Juma Sadi Khamis amesema tukio hilo limetokea leo Jumamosi Oktoba 9, 2021 katika kituo cha kupigia kura cha Msuka Magharibi.
Kamanda Khamisi amesema kijana huyo alitiliwa mashaka na alipopekuliwa akakutwa na misokoto minne ya bangi.
"Yule kijana alifika mara ya kwanza akaondoka bila kupiga kura kisha akarudi mara ya pili lakini akatiliwa shaka ndipo alikamatwa na kuanza kupekuliwa akakutwa na nyongo (misokoto) nne za bangi," amesema Kamanda Khamis.
Hata hivyo, Kamanda Khamis amesema hali ya usalama ni shwari, bado hakujatokea tukio lolote la kuashiria uvunjifu wa amani ukiachilia mbali tukio hilo la bangi.