Bukombe. Mahakama ya Hakimu Mkazi Wilaya ya Bukombe mkoani Geita, imemhukumu kifungo cha maisha jela Juma John (25) mkazi wa Kata ya Masumbwe wilayani hapa baada ya kumtia hatiani kwa kosa la kumbaka mwanafunzi wa darasa la sita Shule ya Msingi Nyakasaluma.
Hukumu hiyo ilitolewa baada ya mtuhumiwa kukiri kutenda kosa hilo.
Akitoa hukumu hiyo Hakimu Mkazi wa mahakama hiyo, Amon Kahimba alisema kwamba anakubaliana na ushahidi uliotolewa na upande wa mashtaka hivyo kumtia hatiani mshitakiwa huyo.
Kabla hajatoa hukumu hiyo, Kaimba alimtaka mshtakiwa kujitetea mbele ya mahakama ambako mshtakiwa aliomba kupunguziwa adhabu.
Awali, mwendesha mashtaka wa polisi wilaya ya Mbogwe, Orgenes Digna aliiambia mahakama kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo Mei 24 mwaka huu mchana kwenye shamba la mihogo.
Digna alidai mshtakiwa kabla hajatenda kosahilo la ubakaji alimuita mwanafunzi huyo akamwambia baba yake mzazi anamdai Sh20,000 anatakiwa akampe nyumbani ili ampelekee baba yake.
Pia Soma
- Profesa Kabudi awatangazia fursa wenye hoteli Dar
- Mume, mke mbaroni kwa madai ya kuua mtoto wao
- Waziri Mbarawa aagiza wakandarasi Mtwara kuwekwa ndani
Pia mwendesha mashitaka alidai kwamba mshtakiwa anatuhumiwa kwa kuwabaka wanafunzi wengine wawili kwa mtindo wa kuwaambia akawape mihogo ya kutafuna.
Alisema mshtakiwa anawashawishi wanafunzi wanapoachiwa shuleni kwenda kula chakula cha mchana na alitenda makosa hayo kati ya Aprili 7 na Juni 12. Hata hivyo mshtakiwa alikana makosa hayo na shauri hilo kuahirishwa hadi Juni 27 mwaka huu.