Tabora. Mkazi wa Majengo wilayani Urambo Mkoa wa Tabora, Seleman Mashaka (31) anatuhumiwa kuwapa sumu watoto wake wa kambo na mmoja kufariki.
Kamanda wa polisi mkoa wa Tabora, Emmanuel Nley amesema amesema leo Jumanne Aprili 30, 2019 kuwa walipata taarifa jana Jumatatu saa 8:00 mchana za mtoto kufariki na mwingine mahututi kutokana na kunywa soda na juisi zinazodhaniwa kuwa na sumu.
Amedai kuwa uchunguzi wa awali umebaini kuwa mtuhumiwa ndiye aliyewanunulia watoto soda na juisi na kuziwekea sumu kwa lengo la kuwaua.
Amedai mtuhumiwa anaishi na mwanamke ambaye ni mama mzazi wa watoto hao wanaodaiwa kuwekewa sumu.
Amemtaja mtoto aliyefariki kuwa ni Nyamizi Ally Ramadhani (7) na aliyelazwa Hospitali ya Wilaya ya Urambo ni Kalunde Ally Ramadhan (4), akibainisha kuwa hali yake ni mbaya.
Akielezea zaidi tukio hilo, Nley amesema mtuhumiwa hakuwa akipenda kuishi na watoto hao na alipenda zaidi kuishi na mama yao, huku akitaka watoto hao wakaishi na baba yao mzazi.
Amesema jana muda usiojulikana Mashaka anadaiwa kuwanunulia watoto hao soda na juisi na kuziwekea sumu ambayo haijajulikana.
Amesema Polisi inamshikilia mtuhumiwa na kwamba, uchunguzi unaendelea.
Naye mganga mkuu wa Wilaya ya Urambo, Dk Paul Swakala amesema mtoto aliyebaki anaendelea na matibabu.