Mwanza. Helena Washera (19) mkazi wa Nyamilamba wilayani Kwimba jijini Mwanza anashikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza akidaiwa kumuua mtoto wake, Abdalah Simon mwenye umri wa miezi tisa kwa kumnyonga kwa kanga ili aolewe.
Taarifa iliyotolewa leo Jumamosi Machi 14, 2020 kwa vyombo vya habari na Kamanda wa polisi Mkoa huo, Jumanne Muliro amesema mama huyo alishirikiana pamoja na mpenzi wake, Lucas Jackson (24) akimlaghai wamuue mtoto huyo ili amuoe.
Kamanda Muliro amesema tukio hilo lilitokea kijiji cha Bugembe Februari 25, 2020.
"Baada ya mama wa mtoto kuelezwa na mpenzi wake (Jackson), kuwa amuue mtoto huyo ili amuoe ndipo walifanya hivyo na kuendeleza uhusiano japo walikuwa hawajaona kama walivyokubaliana," amesema Kamanda Muliro
Amesema baada ya muda kupita baba wa marehemu, James Simon alienda kwa mzazi mwenziye (Helena) kumsalimia mtoto wake lakini aliambiwa kwamba mtoto huyo yupo kwa bibi yake na hata alipokwenda kwa bibi hakumuona ndipo alitoa taarifa polisi.
Amesema baada ya polisi kufuatilia jambo hilo na kuwahoji watuhumiwa wote wawili Machi 12, 2020 walikiri kutenda kosa hilo na kuwapeleka ulipofanyikia unyama huo ambapo walikuta mifupa inayosadikiwa kuwa ya mtoto huyo.
Pia Soma
- Kiongozi wa upinzani Zimbabwe afananisha ukandamizwaji wa demokrasia Afrika na Corona
- Takukuru yaokoa Sh8 bilioni ya vyama vya ushirika
- Itakachokifanya ACT- Wazalendo ikiingia Ikulu 2020