Tabora. Mkazi wa Kata ya Mwaisela wilayani Nzega, Sada Abdallah, anatuhumiwa kumuua mume wake kwa kumpiga na kisha kumsukuma na kuanguka, kutokana na wivu wa kimapenzi.
Kamanda wa polisi Mkoa wa Tabora, Emmanuel Nley, amesema leo Jumatano Mei 29,2019 kuwa tukio hilo limetokea jana, saa tano usiku.
Akielezea tukio hilo, amedai Nicholas Evarist (27) akiwa nyumbani kwake chumbani katika Kata ya Nzega Mashariki, alipigwa na mkewe huyo na kisha kusukumwa na kuangukia kisogo.
Amedai kuwa Nicholaus alifariki dunia katika Hospitali ya Wilaya ya Nzega alipokuwa akipatiwa matibabu.
Amesema chanzo cha tukio hilo ni wivu wa mapenzi baada ya mke kumtuhumu mumewe huyo aliyekuwa fundi wa vioo kuwa na mahusiano na wanawake wengine.
Kamanda Nley, amesema mtuhumiwa Sada anatarajiwa kufikishwa mahakamani upelelezi utakapokuwa umekamilika.
Pia Soma
- Mivutano ya wazazi yawashindisha njaa wanafunzi
- Shambulizi la kisu laua watatu Japan
- Viongozi wa umma watakiwa kuzingatia maadili
Amesema wapo baadhi ya watu huchonganisha wana ndoa wakiwa na malengo yao na kuonya wana ndoa kuwa makini na maneno kutoka kwa watu wasiozitakia mema ndoa za wengine.