Musoma. Polisi mkoani Mara nchini Tanzania linamsaka, Juma Warioba (27) mkazi wa kijiji cha Wegero wilayani Butiama kwa tuhuma za kumuua mke wake baada ya kutokea ugomvi kati yao uliotokana na wivu wa kimapenzi.
Warioba anatuhumiwa kumuua mke wake, Devotha Boniface (22) kwa kumchoma na kisu sehemu mbalimbali za mwili wake na kusababisha kifo chake papo hapo akimtuhumu kuwa na mahusiano na wanaume wengine.
Kamanda wa polisi mkoa wa Mara, Daniel Shillah amesema tukio hilo limetokea jana Alhamisi Januari 9, 2020 saa 4 usiku kijijini kwao Wegero.
Kamanda Shillah amesema taarifa za awali zinaonyesha mwanaume huyo tangu walipofunga ndoa na mke wake Septemba 2019 amekuwa akimtuhumu mke wake kutokuwa mwaminifu katika ndoa yao.
Amewataka wakazi wa mkoa wa Mara hususan wanaume kuachana na vitendo vya ukatili na kwamba endapo kutatokea kutokuelewana ni vema wakaamua kuvunja mahusiano au kuomba usuluhishi kutoka kwa watu wanaowaamini.
"Hivi inakuwaje unaamua kumuua mwenzio kisa tu unadhani sio mwaminifu, kama mmeshindana kwa nini msiachane kwa amani? Ona sasa amekatisha maisha ya mwenzi wake nasi tunamtafuta na lazima tutampata tu na kumfikisha kwenye vyombo vya sheria," amesema kamanda Shillah.