Shinyanga. Shaibu Hamis mkazi wa mtaa wa Mabambase manispaa ya Shinyanga anadaiwa kujeruhiwa sehemu za siri kwa wembe na mpenzi wake baada ya kumnyima fedha.
Tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia leo Jumatano Aprili 8, 2020 saa 7 usiku nyumbani kwa Shaibu.
Taarifa zilizolifikia Mwananchi zinaeleza kuwa wawili hao walitoka katika kilabu cha pombe na baada ya kuingia ndani ukaibuka ugomvi.
Mwenyekiti wa mtaa wa Mabambase, Bakari Hamis amesema wawili hao waligombana na mwanamke aliyedai jina lake halijafahamika alichukua wembe na kumkata Shaibu sehemu za siri kwa madai kuwa alimuomba fedha lakini akamnyima.
“Walifika nyumbani kwangu saa saba usiku wakiwa wamefuatana na majirani na aliyejeruhiwa. Niliwapokea na kusikiliza maelezo yao kisha nikawapatia barua ili wawahi kwenye matibabu, pia nikatoa taarifa polisi kuhusu tukio hilo.”
“Kwa sasa majeruhi anaendelea vizuri. Alikwenda hospitali ya rufaa ya Mkoa ambako alitibiwa na kuruhusiwa kurejea nyumbani, katika maelezo sababu ilikuwa ni kuomba fedha na kunyimwa,” amesema mwenyekiti huyo wa mtaa.
Pia Soma
- Waziri asimamishwa kazi kwa kukiuka amri ya kutotoka nje
- Walioambukizwa corona Tanzania wafikia 25
- Kina Mbowe wakata rufaa Mahakama Kuu