Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kamanda wa Polisi wa mkoa huo, Henry Mwaibambe, alisema tukio hilo limetokea Juni 28, mwaka huu katika Kijiji cha Bokondo, Tarafa ya Butundwe, Wilaya ya Geita.
Kamanda Mwaibambe alisema, Budagala aliuawa kwa kukatwa na mapanga shingoni na watu wasiojulikana baada ya kumkuta mama yake mzazi akifanya mapenzi na mwanamume mwingine, wakati baba yake mzazi akiwa safarini mkoani Kagera.
Alisema kiini cha tukio hilo ni mgogoro wa kifamilia, baada ya baba wa marehemu, Vita Bupilipili, kusafiri kwenda kutafuta maisha Juni 26, mwaka huu na kumuacha mke wake pamoja na mtoto wake huyo.
Alisema Budagala alimkuta mama yake mzazi akifanya mapenzi na mwanamume mwingine nyumbani kwao na kusababisha mgogoro ndani ya familia hiyo.
Alisema baada ya tukio hilo, mama mzazi wa marehemu alikimbia na kutokomea kusikojulikana na anatafutwa na Jeshi la Polisi ili sheria iweze kuchukua mkondo wake.
Kadhalika, polisi inawashikilia watu watano kwa ajili ya mahojiano kuhusiana na tukio hilo. Majina ya watuhumiwa wote yamehifadhiwa kwa ajili ya uchunguzi.
Kamanda aliwataka wananchi wa mkoa huo kuacha tabia ya kujichukulia sheria mkononi kwa kuripoti matukio yote ya uhalifu katika vyombo vya sheria.
“Kwa umoja wetu tunaweza kutokomeza uhalifu,” alisema.