Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Jumanne Muliro amesema jeshi hilo limenasa watuhumiwa 91 wanaojihusisha na makosa ya wizi na unyang’anyi wa magari na kusafirisha na kuuza dawa za kulevya.
Amesema kukamatwa kwa watuhumiwa hao ni mafanikio ya operasheni waliyofanya tangu Januari Mosi hadi 12, 2022 na kwamba jeshi hilo linatambua mwezi huo watu wanadai ni mgumu hivyo baadhi yao wanatumia nafasi hiyo kujihusisha na matukio ya kihalifu.
Akizungunza Dar es Salaam leo Alhamisi Januari 20, 2022, Kamanda Muliro amesema watuhumiwa wengine walionaswa kwenye operesheni hiyo ni matapeli wanaojifanya maofisa wa serikali.
“Januari huwa kuna tabia ya watu kudai kwamba ni ngumu hivyo baadhi ya watu wanajikita kwenye vitendo vya kufanya uhalifu bila kutambua kuwa jeshi hilo limekuwa na operesheni kali dhidi ya watu wanaopanga njama kuhakikisha wanakamatwa na kuingizwa kwenye mifumo ya kisheria ili haki itendeke.
“Katika operasheni hiyo watuhumiwa 91 watapelekwa kwenye mifumo ya kisheria ili haki itendeke na mali tulizokamata zitaambatanishwa kwenye vielelezo vya ushahidi mahakamani,”amesema Kamanda Muliro
Kamanda huyo katika maelezo yake amefafanua kuwa katika operasheni hiyo pikipiki zaidi ya 12 ambazo zilihusishwa na watuhumiwa wa unyang’anyi wa kutumia nguvu kwa kujifanya wanakodi pikipiki na kuwapeleka maeneo ambayo yako mbali na makazi ya watu na baadae biria kugeuka mualifu.
“Matapeli wengine tuliowakamata ni wale wanaojifanya maofisa wa serikali na wanapita kwenye ofisini kuwatapeli watu kwamba wanaweza kuwafanyia mipango mbalimbali ya kazi lakini kuwachukulia fedha na kinara wao mmoja tumemkamata,”amesema
Amesema mali zingine walizonasa kupitia operesheni hiyo ni pamoja na vifaa vya majumbani ikiwamo majenereta ,televisheni na redio ambavyo vitapelekwa kama sehemu ya vielelezo vitakavyosaidia upelelezi mahakamani.
Aidha Jeshi hilo limetoa wito kwamba halitasita kutumia mifumo yake ya kiutendaji kufuatilia kwa siri lakini kushirikiana na wananchi wema kuhakikisha watuhumiwa wanaopanga njama za kufanya uhalifu wanakamatwa kabla ya kutenda vitendo hivyo.
“Tukipata taarifa tutafanya kila namna kuwakamata kabla mali walizoiba hazijawanufaisha na zinatumika mahakamani kama vielelezo kwahiyo natoa wito ni hatari sana kuelekeza akili yako katika mfumo wa vitendo vya kialifu ikiwemo unyang’anyi wa kutumia silaha au nguvu ,”amesema