WATU 11 wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam wakikabiliwa na shitaka la kusafirisha kilogramu 20.24 za dawa za kulevya aina ya heroin.
Washitakiwa hao Silvanus Mkasanga, Ally Juma, Rifat Omary, Haruna Salu, Godlisten Mamba, Frola Mamba, Khamis Khamis, Yuda Muhagama, Justine Mnyalape, Emmanuel Mgeni na Mikidadi Nyangale walipandishwa kizimbani jana.
Akiwasomea shitaka hilo mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi, Yusto Ruboroga, Wakili wa Serikali, Yusuph Aboud, alidai kuwa Aprili 29, 2021 katika eneo la Sangasanga Check Point, Wilaya ya Mvomero Mkoa wa Morogoro, washitakiwa hao walikutwa wakisafirisha dawa hizo haramu.
Wakili Aboud aliieleza Mahakama kuwa, upelelezi wa kesi hiyo haujakamilika hivyo alioomba tarehe nyingine ya kutajwa. Kesi hiyo iliahirishwa hadi Mei 26, mwaka huu.