Shirika la Bima Zanzibar (ZIC) limewakaribisha wawekezaji kuja kuwekeza visiwani Zanzibar na kuwahakikishia usalama wa mali zao wakati wote watakapokuwa visiwani humo.
Akizungumza katika Maonesho ya Biashara ya Kimataifa (Dubai Expo) yanayoendelea nchini Dubai, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la ZIC, Arafat Haji aliwakaribisha wadau kuwekeza visiwani Zanzibar na kuwa shirika hilo linawahakikishia usalama wawekezaji kwani shirika hilo lina uzoefu wa masuala ya bima za aina mbalimbali.
“Wawekezaji tunawapa elimu ya namna gani wataweza kuwa na uwekezaji wenye usalama na kuhakikisha kunakuwa na ajira ya muda mrefu ili kuleta tija na kukuza uchumi na maslahi ya Taifa,” alisema.
Aidha, Haji ameeleza kuwa wawekezaji wanapoamua kushirikisha ZIC inafanya maamuzi sahihi kwani ipo tayari kuwapa miongozo ya kusimamia uwekezaji huo na kuhakikisha mitaji yao inaleta manufaa.