Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Maendeleo ya Mazao kutoka Wizara ya Kilimo, Beatus Malema ameyasema hayo leo mkoani Mbeya wakati wa kikao cha wadau wa zao la Kahawa ambacho kiliwahusisha, wakulima kutoka mikoa ya Ruvuma, Songwe na Mbeya, mameneja wa bodi wa zao hilo.
Kikao hicho ambacho kiliandaliwa na Taasisi ya Cafe Afrika, kilikuwa na lengo kuwakutanisha wadau wa kahawa ili kuboresha mnyororo wa thamani wa zao hilo ambao utawasaidia wakulima na wafanyabiashara kukabiliana na vikwazo ikiwemo soko la uhakika na usimamizi mzuri wa vyama vya ushirika.
Malema, amesema baadhi ya warajisi wamekuwa sehemu ya tatizo kwani wameshindwa kusimamia ipasavyo majukumu yao na ikiwemo kushughulikia migogoro kwa wakulima walijiunga kwenye AMCOS hali inayosababisha wakulima kufikisha malalamiko yao Wizara ya Kilimo.
“Serikali imeajiri warajisi kwa ajili ya kufuatilia na kutatua kero za wakulima walio kwenye AMCOS na si kukaa maofisini lakini sio kama ilivyo sasa kumekuwa na malalamiko mengi kutoka kwa wakulima ambao hufika wizarani kuhitaji msaada wakati nyie mko kwenye maeneo hayo mmekuwa sehemu ya migogoro na ubadhilifu naomba mbadilike mara moja,” amesema Malema.
Hata hivyo Malema, ameagiza Bodi za Kahawa nchini kujitathimini na kuweka mikakati kuhakikisha wanaongeza tija kuboresha uzalishaji wa miche bora ya zao kahawa baada ya kuporomoka kwa ubora wa zao na kuathiri soko la ndani na nje ya nchi.
Mikakati ya Serikali sasa ni kutoa kipaumbele kwa zao la Kahawa ili kuongeza tija ya uwepo wa masoko ya dunia na sambamba na kutoa teknolojia za kisasa ili uzalishaji wa Kahawa ukidhi mahitaji ya soko la dunia na kumnufaisha mkulima.
Mkurugenzi wa Taasisi ya Cafe Afrika, ,Dafosa Sanga, amesema kuwa lengo la mkutano huu ni kuwezesha bodi zinazosimamia wakulima wa kahawa kuboresha thamani ya zao hilo katika mnyororo wa thamani na kuboresha kiwango cha uzalishaji ili kuwasaidia wakulima waliojiunga kwenye vyama vya ushirika.
Amesema kwa mwaka 2020/2021 jumla ya wakulima 6,000 wamefikiwa na elimu ya uzalishaji bora wa kahawa na kwamba lengo ni kuwafikia wakulima 24,000 wa kahawa nchini hususani kuwapatia elimu ya kilimo bora ,upatikanaji wa pembejeo za kilimo sambamba na kukarabati mitambo 20 kwenye AMCOS.
Mkurugenzi wa Maendeleo ya Kahawa nchini (TCB) Kajivu Kisenge, amesema kuwa Tanzania inakabiliwa na kikwazo cha kuporomoka kwa uzalishaji zao hilo na kwamba kupitia kikao hicho bodi za kahawa hazina budi kukaa meza moja na kuweka mikakati ya namna kilimo hicho kitakuwa na thamani na kuwanufaisha wakulima.
Miongoni mwa wakulima wa kahawa kutoka wilayani Mbozi katika Mkoa wa Songwe alisema kwa kiasi kikubwa wanategemea mvua hivyo anapendekeza kuandaa sera ya maji kwenye maeneo ya milima kutengeneza mifumo ya ufikishaji wa rasimali hiyo kutoka katika mito ambayo itawawezesha kuzalisha kwa tija kutokana mabadiliko ya tabia nchi.