Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Wizara kuimarisha huduma uogeshaji mifugo

Majosho Sababaa Wizara kuimarisha huduma uogeshaji mifugo

Fri, 10 Mar 2023 Chanzo: Habarileo

MTENDAJI Mkuu wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA), Dk Stella Bitanyi amesema Wizara ya Mifugo na Uvuvi hivi sasa ina mkakati wa kuimarisha huduma za uogeshaji wa mifugo kwa kuwezesha halmashauri kujenga majosho nchi nzima.

Dk Bitanyi amesema hayo alipokuwa akizungumza na HabariLeo kuhusu wizara hiyo kupitia TVLA.

Amesema kila halmashauri ikiwa na majosho wakala utaendelea kuhakiki ubora wa hizo dawa za kuogeshea mifugo.

“Kwa hiyo sasa hivi mkakati wa wizara ni kuimarisha hizi huduma za uogeshaji kupitia kuwezesha halmashauri kujenga majosho nchi nzim na kila kata ikiwezekana kupata majosho na sisi tunaendelea kuhakiki ubora wa hizo dawa.

“Kuna utaratibu wa kuweka dawa kwenye majosho, baada ya muda, baada ya michovyo Fulani kuna kuongeza nguvu. Ili kuendelea kudhibiti wale kupe lazima sampuli zichukuliwe zipimwe kujua kama uwezo umeshuka kujua sasa ni wakati sahihi wa kuongeza dawa nyingine,” amesema.

Kwa maelezo yake dawa ikishaongezwa mara kadhaa inabidi yale maji yote yatolewe na kuwekwa maji mapya na dawa mpya.

“Ni mkakati wa serikali katika kudhibiti magonjwa. Kuna mkakati wa kudhibiti magonjwa yanayoletwa na kupe pamoja na ndorobo,” amesema.

Aliongeza kuwa magonjwa ya ndibana kali yanayoletwa na kupe yanaua mifugo na matibabu yake ni ghali hivyo kinga ni bora kuliko tiba.

Chanzo: Habarileo