Dar es Salaam. Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amezitaka kampuni binafsi kuchangamkia fursa za ujenzi wa miradi mikubwa inayotekelezwa nchini.
Majaliwa ameyasema hayo leo Agosti 29, 2018 akiwa Ubungo jijini Dar es Salaam kukagua ujenzi wa barabara za juu (Interchange)
Amesema Serikali ikijiimarisha, basi sekta binafsi zinaweza kuchangamkia zabuni za kutoa huduma na malighafi.
"Sisi tumewahakikishia tutakuwa bega kwa bega na kampuni zetu za ndani, zije katika miradi hii mikubwa ili baadaye tutakapotangaza ujenzi wa barabara za juu zijengwe na Watanzania wenzetu," amesema.
Amesema alikwenda kutembelea ujenzi wa barabara hizo na ameridhishwa na utendaji ikiwamo uwepo wa vifaa vya kutosha na amehakikishiwa na wahandisi kuwa mradi utakamilika kwa wakati.
Amesema hadi Juni mwaka 2020 barabara hiyo itakuwa imekamilika na kuanza kutumika ili yale ambayo Rais John Magufuli aliyaahidi yawe yametekelezwa.