Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema ameridhishwa na maendeleo ya mradi wa ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) na kwamba Serikali itaendelea kuhakikisha mradi huo unajengwa kwa viwango na kukamilika kama ilivyobainishwa kwenye mkataba.
Amesema kuwa ujenzi wa reli hiyo unaendelea vizuri katika vipande vyote na kwamba Serikali itahakikisha mradi huo haukwami na itakabiliana na viashiria vyote vinavyoweza kukwamisha utekelezaji wake.
Ameyasema hayo jana, Novemba 24, 2022 wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa stesheni kuu ya Dodoma katika eneo la Mkonze, jijini Dodoma.
Akizungumza baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa stesheni hiyo, Majaliwa amewataka Watanzania wanaoshiriki katika ujenzi wa mradi huo wasimamie usalama wa mradi na wawe walinzi ili ukamilike kama ilivyokusudiwa.