Dodoma. Waziri wa Madini, Doto Biteko amesema suala la usafirishaji wa mchanga wa madini ya dhahabu ‘makinikia’ nje ya nchi limekwama kutokana na sababu za kisheria na kulieleza Bunge kwa sasa hawezi kuondoa zuio hilo.
Biteko amesema hayo leo Jumatatu Mei 27, 2019 wakati akihitimisha hoja aliyoiwasilisha asubuhi ya makadirio ya mapato na matumizi ya wizara yake kwa mwaka 2019/20 ya Sh49.46 bilioni.
Hoja hiyo imechangiwa na wabunge 10 wa kuzungumza na wabunge 18 wamechangia kwa maandishi.
Waziri huyo akizungumzia zuio la makinikia kwenda nje, amesema, “Tunayo changamoto ya kisheria, tunaifanyia kazi, tunahitaji mapato, lakini tunahitaji kuwa makini na tunalimaliza hili jambo.”
Amesema kuna sehemu tumekwama, hata leo nikisimama nikasema anza kusafirisha makinikia, anayesafirisha atakwama na kukutana na hasara kubwa.
Kuhusu tozo zinazotozwa kinyume cha sheria ambazo Bunge limekwisha kuzifuta, Waziri Biteko amesema, “Mtu yeyote anayetoza kodi wakati Bunge limefuta tutachukua hatua na tutaendelea kulifanyia kazi kwa nguvu zote na kama kuna majina ya watu wanaotoza kodi hizo, mtuletee tutachukua hatua.”
Pia Soma
- MADAI: DPP awatuhumu wabunge kwa rushwa, Spika ajibu
- DC atangaza operesheni tokomeza wanaume teleza
- Wapinzani waibuka na makinikia bungeni
Awali, akijibu hoja za wabunge, Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo alisema uanzishwaji wa masoko ya madini yatasaidia kuongeza mapato na kuzuia utoroshwaji.
Amesema siku ya kwanza walipofungua soko la Chunya waliweza kupata kilo 13 za dhahabu. “Tulipata zaidi ya Sh68 milioni na masoko zaidi ya 20 yamefunguliwa.”
Nyongo ambaye pia ni Mbunge wa Maswa Mashariki (CCM), amesema hadi leo, kilo 578 zimeuzwa kwenye masoko hayo na Serikali imepata mrabaha wa Sh3.6 bilioni.
“Tukiendelea kusimamia vyema haya masoko tutapata fedha nyingi,” amesema Nyongo