Tanga. Waziri wa Madini nchini Tanzania, Dotto Biteko amewaagiza watumishi wa wizara yake kutokuwa wepesi kufungia migodi au kuwakwamisha wachimbaji wadogo wa madini, kuwataka kutoa mwongozo namna ya kujikwamua.
Ametoa kauli hiyo leo Jumamosi Agosti 31, 2019 mjini Tanga katika mkutano wa sita wa Shirikisho la Vyama vya Wachimbaji Madini Tanzania (Femata).
Amesema watumishi wa wizara yake wanapaswa kutambua sekta ya madini imebeba maisha ya mamilioni ya Watanzania, kwamba wanapotaka kutoa uamuzi wanapaswa kufikiri zaidi.
"Wachimbaji madini wanatakiwa kupewa elimu na kuonyeshwa njia ya kupita na si kufungia mgodi au kuwanyanyasa wanapokosea," amesema Biteko.
Amesema sekta hiyo imetoa ajira kwa Watanzania wengi, inapaswa kuangaliwa kwa makini.
Rais wa Femata, John Bina amesema kuna baadhi ya watumishi wa Serikali hawajatambua kuwa baadhi ya kodi zimefutwa, kwamba wanatakiwa kuelimishwa.
Pia Soma
- Alichokisema Lugola kuhusu wahamiaji haramu
- RC Mghwira ataka nyuki kutumika kuwaondoa tembo waliovamia makazi ya watu
- Mvua yazua jambo Serengeti, yaezua paa shule ya msingi Singisi
Makamu Mwenyekiti wa chama cha wafanyabiashara wa madini nchini (Tamida), Thomas Munisi amewapongeza Femata kwa kuandaa mkutano huo kwa maelezo kuwa unachochea maendeleo ya sekta hiyo.
"Tutaendelea kushirikiana kwenye sekta ya madini kwa lengo la kuhakikisha wadau wanafaidika na Serikali inachukua kodi," amesema Munishi.