Dodoma. Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu nchini Tanzania (Uwekezaji), Angela Kairuki amesema wamejitokeza wawekezaji wawili wa bangi ambao lengo lao ni kuchakata mafuta yanayotokana na zao hilo.
Kairuki ameeleza hayo leo Jumatatu Februari 3, 2020 bungeni mjini Dodoma wakati akitoa taarifa baada ya Mbunge wa Kahama Mjini (CCM), Jumanne Kishimba kuomba Serikali kuruhusu kilimo hicho.
Katika maelezo yake, Kairuki amesema tayari wamepata wawekezaji wawili wanaotaka kuwekeza katika kilimo cha bangi ila hitaji lao ni kupata mafuta ya bangi yanayotumika kwenye matibabu.
“Tunaendelea kufanyia kazi kama Serikali kwa sababu bado hakuna mwongozo kuweza kuona kama itakubalika ama la,” amesema.
Amemtaka mbunge huyo kuwaachia mamlaka zinazohusika kulishughulikia jambo hilo.
Akimpa taarifa Kishimba, Mbunge wa Geita Vijijini (CCM), Joseph Musukuma amesema kwa kuwa sheria ya kilimo hicho ipo kinachofuata ni kutunga kanuni.