SERIKALI imefungua mlango kwa mwekezaji anayetaka kuwekeza kwa ubia na serikali kwenye Kiwanda cha kutengeneza dawa (TPI) kilichopo Arusha.
Uwekezaji huo wa ubia utakuwa asilimia 30 kwa serikali na asilimia 70 kwa mwekezaji. Hayo yamebainishwa leo na Naibu Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe wakati akijibu kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara swali la Mbunge wa Arusha Mjini Mrisho Gambo (CCM).
Bashe alisema ni dhamira ya serikali kuhakikisha kiwanda hicho kinafufuliwa. Aidha Bashe amesema pia Serikali inatambua umuhimu wa kuwa na viwanda mbalimbali nchini vikiwemo viwanda vya matairi na dawa ili kuchochea uchumi wa nchi kwa kuzalisha bidhaa na ajira.
Amesema Kiwanda cha Matairi kilichojulikana kama General Tyre Arusha lakini kwa sasa kinajulikana kama Kiwanda cha Matairi Arusha, ni moja ya kiwanda kikubwa cha matairi katika ukanda wa Afrika Mashariki.
“Uzalishaji katika kiwanda hicho ulisimama mwezi Agosti 2007 baada ya kukosa fedha za kujiendesha hususan fedha za kununua malighafi, hivyo, Wizara imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za kukifufua kiwanda hicho ili kufikia malengo ya serikali ya kujitosheleza kwa mahitaji ya matairi nchini, kuokoa fedha za kigeni zinazotumika kuagiza matairi kutoka nje na kuzalisha ajira,”amesema Bashe.
Bashe amesema wizara kupitia Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC) iliunda Timu ya Wataalamu ili kufanya tathmini kuhusu njia bora ya kuendesha kiwanda hicho.