Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Watumishi TRA wapewa funzo hili

TRA Watumishi TRA wapewa funzo hili

Sun, 5 Nov 2023 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

WATUMISHI wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Shinyanga wametakiwa kuwa na maadili, kuficha siri, kuwa na matumizi bora ya fedha na nyaraka, lugha nzuri kwa wateja wao na kufuata misingi ya kazi.

Hayo yalisemwa November 4, 2023 na Katibu Msaidizi, ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda ya Magharibi, Gerald Mwaitebele alipokuwa akitoa mafunzo ya maadili kwa watumishi hao kwa lengo la kuwakumbusha wajibu.

Mwaitebele aliwasisitiza watumishi hao kubadilisha tabia, matumizi mabaya ya lugha kwa wanaowahudumia, kuacha kuomba rushwa, kukopa bila kulipa, kutoa siri za ofisi na kuihujumu Mamlaka badala yake wawe waadilifu ndani na nje ya ofisi .

“Kuanzia sasa tubadilishe mwenendo wetu, tubadili tabia zetu, matumizi ya lugha kwa tunaowahudumia ambao ndiyo umma, tuanze kuyaishi maadili kuanzia leo na tukumbuke kuwa sisi ni viongozi tunaotumikia umma hivyo tunatakiwa kuwa kioo mbele ya umma”. alisema Mwaitebele.

Mwaitebele alitaja miongoni mwa sifa na utambulisho wa mtumishi mwadilifu kwa umma ikiwemo pamoja na kujali wengine wakati wote, kujitolea kusaidia wenye uhitaji bila kujali kama anacho au hana, kuwa msikivu, mwaminifu nyakati zote na anayeheshimu kila mtu bila ubaguzi.

“Sifa nyingine ni pamoja na kuwa mnyenyekevu, kufanya kazi kwa bidii, kutenda haki, anapaswa kufikiria kwa makini kabla ya kutenda, kujizuia na tamaa ya aina yoyote na kuwa tayari na kukubali kukoselewa na kubadilika”alisema Mwaitebele.

Mwaitebele akitoa mfano wa kutoa siri za mikakati ya TRA kwa wateja kwa maslahi binafsi , kutoa nyaraka na kumpa mteja au kiongozi wa chama cha kisiasa bila kufuata utaratibu hapo utakuwa umekiuka misingi ya maadili ya utumishi wa umma.

Meneja TRA mkoa wa Shinyanga Faustine Mdessa alisema wao kama watumishi na viongozi wa umma wapo tayari kupokea mafunzo ya maadili ya viongozi wa umma, wapo tayari kupokea maelekezo, miongozo na ushauri wote watakaopewa na kuahidi kutekeleza maadili kwa vitendo.

Aidha sekretarieti imeanzishwa kwa mujibu wa Ibara ya 132 ya katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma ya mwaka 1995,

Chanzo: www.tanzaniaweb.live