Simanjiro. Watumishi zaidi ya 40 wa Wizara ya Madini wamechukuliwa hatua mbalimbali za kinidhamu ikiwamo kuhamishwa vituo vya kazi, kusimamishwa na kufukuzwa kazi baada ya kubainika kuzembea au kushirikiana na watoroshaji wa madini nje ya nchi.
Waziri wa Madini Angellah Kairuki ameyasema hayo leo Agosti 2 katika ziara yake wilayani hapa wakati akikagua utendaji kazi kwenye mgodi wa madini ya Kinywe (Graphite) unaomilikiwa na kampuni ya Godmwanga Gems Limited eneo la Mirerani kuwa uamuzi huo umechukuliwa ili kutoa onyo kwa watumishi wasio waaminifu.
Amesema serikali haitawavumilia watumishi wanaoshirikiana na wafanyabiashara wasio na uzalendo wa kulipa kodi na tozo mbalimbali na kuwataka wananchi kutoa ushirikiano kwa serikali kuwafichua wanakwamisha juhudi za serikali kuongeza mapato.
Kuhusu kuimarisha usalama katika mgodi wa madini ya Tanzanite ambao umewekewa ukuta ili kulinda rasilimali hiyo inayopatikana hapa nchini pekee amesema hawezi kuzungumzia kinagaubaga mbinu zinazotumika kulinda eneo hilo.
“Suala la ulinzi wa eneo hili ni muhimu sana sio kila kitu tutakizungumza ila niwatangazie kiama wafanyabiashara waliozoea kutorosha madini yetu nje ya nchi haitakua tena vile walivyozoea,niwashauri wafuate taratibu kwa kulipa kodi na tozo zinazostahili,”amesema Kairuki