Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Watanzania watumia Sh6 trilioni kupiga simu, kutuma sms

12317 Pic+simu TanzaniaWeb

Fri, 17 Aug 2018 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dar es Salaam. Watanzania milioni 41 wanaomiliki simu za mezani na mkononi wametumia zaidi ya Sh6 trilioni kwa ajili ya kulipia muda wa maongezi ndani na nje ya nchi na kutuma ujumbe mfupi (sms).

Hata hivyo, kiwango hicho kinaweza kupungua kutokana na baadhi ya mitandao ya simu kuwa na vifurushi vya maongezi na sms ambavyo ni kwa ajili ya promosheni ya kuvutia wateja zaidi.

Kiasi hicho cha matumizi kilirekodiwa kwenye robo ya pili ya mwaka iliyoishia Juni ni kikubwa ikilinganishwa na Sh4.8 trilioni zilizotumika katika kipindi kama hicho mwaka jana.

Kuongezeka kwa kiasi hicho ni kutokana na ongezeko la muda wa kupiga simu (dakika) na idadi ya ujumbe mfupi. Gharama nyingi isipokuwa kupiga simu nje ya nchi zilipungua katika vipindi hivyo vilivyofanyiwa uchambuzi.

Ripoti ya mawasiliano kwa robo ya pili ya mwaka iliyotolewa na Mamlaka ya Mawasiliano (TCRA), inaonyesha mpaka sasa jumla ya watu milioni 41.8 wanatumia simu tofauti na kipindi kama hiki mwaka uliopita ambapo watumiaji walikuwa milioni 40.3.

Katika kipindi kilichoishia Juni 30, Sh4.4 trilioni zilitumika kama gharama ya muda wa maongezi, huku Sh1.7 zikiwa ni gharama ya kutuma ujumbe mfupi wa maandishi.

Kipindi kama hicho mwaka jana, matumizi ya muda wa maongezi yalikuwa Sh3.6 trilioni na Sh1.2 trilioni kwa ujumbe mfupi.

Ripoti hiyo iliyotolewa mwanzoni mwa juma hili inaonyesha katika kipindi cha miezi mitatu (Aprili – Juni) watumiaji wa simu nchini walipiga simu zenye jumla ya dakika bilioni 15.1 ndani na nje ya nchi, sawa na saa milioni 253.14.

Katika muda huo, Sh3.7 trilioni zilitumika kwa simu ndani ya mtandao husika; Sh733 bilioni zilitumika kwa simu zilizopigwa kwenda mitandao mingine; Sh3 bilioni ni gharama ya simu zilizopigwa kwenda nchi za Afrika Mashariki na Sh20 bilioni zilitumika kwa simu zilizokwenda mataifa mengine.

Kwa ujumbe mfupi, jumla ya sms bilioni 23.1 zilitumwa na watumiaji wa simu. Kiwango hicho kimeongezeka kutoa sms bilioni 18.8 zilizotumwa katika kipindi kama hicho mwaka jana.

Ripoti pia imeonyesha kuongezeka kwa matumizi ya huduma ya fedha miongoni mwa watumiaji wa simu za mkononi. Wateja wapya milioni 1.54 wamejiunga na huduma hiyo kupitia mitandao mbalimbali katika kipindi cha miezi mitatu tangu Machi.

Watumiaji wa huduma za fedha za simu za mikononi sasa wamefikia milioni 20.8 kati ya watumiaji milioni 41.8 wa simu za mkononi. Mitandao inayotoa huduma ya miamala ya fedha nchini na viwango kwa asilimia ni Vodacom (Mpesa- asilimia 41), Tigo (Tigo pesa - asilimia 33), Airtel (Airtel Money -asilimia 20), Halotel (Halopesa -asilimia 2), Zantel (Ezy Pesa -asilimia 2) na TTCL (TTCL pesa -asilimia 0.47).

Mtandao unaongoza kwa kuwa na watumiaji wengi wa simu za mkononi nchini ni Vodacom ukiwa na watumiaji milioni 13.2; Tigo (milioni 12.0), Airtel (milioni 11.1), Halotel (milioni 3.6) na Zantel (milioni 1.0).

Chanzo: mwananchi.co.tz