Dar es Salaam. Waziri wa Madini Dotto Biteko amewataka Watanzania kupingana na watu wanaotorosha madini na kuhakikisha wanashiriki kikamilifu katika kulinda rasilimali hiyo.
Amesema anatamani kuona watanzania wanabadilisha maisha yao kupitia madini na sio kuruhusu rasilimali hiyo kuwanufaisha watu wa nje.
Biteko ametoa kauli hiyo leo Ijumaa Julai 5, 2019 katika Uwanja wa ndege wa Chato wakati wakisubiri kumpokea Rais wa Kenya, Uhuru Kenyata ambaye anatarajiwa kuwasili nchini leo kwa ziara binafsi ya siku mbili.
Akizungumza uwanjani hapo, Biteko amesema jitihada zimeendelea kufanyika katika kuhakikisha madini yananufaisha taifa na watanzania.
Amesema jitihada hizo zinawapa matumaini kuwa kwa mwaka huu wataweza kukusanya zaidi ya Sh400 bilioni kutokana na sekta hiyo.
“Hakuna heshima unayoipata kwa kutorosha madini nje ya nchi hiyo ni rasilimali yetu, inapaswa kutunufaisha watanzania na taifa kwa ujumla, unaibiaje nchi yako,” amesema Biteko.