Kama wewe ni msanii au Mwanasiasa na ungetaka jina lako apewe mnyama fulani mfano Simba, Tembo nk. Basi ondoa shaka juu ya hilo kwani linawezekana.
Habari nzuri ni kwamba, Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) imeanza kuandaa utaratibu wa kisheria utakaowawezesha watu maarufu wanaotaka majina yao waitwe wanyamapori wa hifadhi hiyo kuweza kulipia.
Hayo yamesemwa na Mhifadhi mkuu wa mamlaka hiyo, Dkt. Fredy Manongi jana Januari 22, 2018 akiwa na na wajumbe wa kamati ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii waliotembelea hifadhi hiyo na kudai kuwa utaratibu huo utasaidia kuongeza mapato ya Ngorongoro.
Dkt. Manongi amesema wakati utaratibu huo ukifanyika hakuna majina mapya ambayo yatatolewa.
Awali MbungeĀ wa Arumeru Mashariki (Chadema), Joshua Nassari na Joseph Msukuma (Geita Mjini) waliotaka kujua mchakato wa wanyamapori kupewa majina ya viongozi wa kisiasa.
Nassari amesema amepata taarifa kwamba kuna faru anaitwa Ndugai (Job-Spika wa Bunge), kutaka kujua sababu za kupewa jina hilo.
Akitoa ufafanuzi wa jambo hilo, Manongi amesema faru huyo kuitwa Ndugai kunatokana na Spika huyo wa Bunge kuwa mhifadhi, pia alikuwa mjumbe wa bodi ya Ngorongoro kwa muda mrefu.
Chanzo:Mwananchi