Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amewataka wamiliki wa malori nchini wawajali madereva na wahudumu wa magari hayo ikiwa ni pamoja na kuboresha maslahi yao.
Amesema uanzishwaji wa kanzidata ya taarifa za madereva utawawezesha wamiliki hao kutumia taarifa hizo kwa lengo la kusimamia usalama wa madereva pamoja na kufuatilia mienendo na ufanisi wao.
Ametoa wito huo wakati akizungumza na wadau wa sekta ya usafirishaji waliohudhuria uzinduzi wa kanzidata ya madereva wa malori nchini uliofanyika jijini Dar es Salaam.
Kanzidata hiyo imeandaliwa na Chama cha Wamiliki wa Malori Tanzania (TATOA).
Akizungumza na wadau wa sekta hiyo, Waziri Mkuu amesema azma ya Serikali ya awamu ya sita ni kuendeleza sekta hiyo ili iweze kuharakisha ukuaji wa uchumi.