Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Wakulima wa mbaazi wavuna Bil. 1.6

Wakulima Wa Mbaazi Wavuna Bil. 1.6 Wakulima wa mbaazi wavuna Bil. 1.6

Sun, 13 Aug 2023 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Tani 824 sawa na kilo 824,941 zenye thamani ya Sh.bilioni 1,663,081,056 za zao la mbaazi zimenunuliwa kupitia mfumo wa stakabadhi ghalani katika mnada wa kwanza wa zao hilo uliofanyika katika kijiji cha Majimaji wilayani Tunduru.

Katika mnada huo makampuni ishirini yalijitokeza kuomba kununua mbaazi za wakulima,hata hivyo ni makampuni matatu ndiyo yaliyofanikiwa kununua mbaazi zote zilizokusanywa na chama cha msingi cha Majimaji kutoka kwa wakulima kwa bei ya Sh.2,016 kwa kilo moja.

Akizungumza na wakulima mwenyekiti wa Chama kikuu cha Ushirika wilaya ya Tunduru(Tamcu Ltd)Mussa Manjaule amewapongeza wakulima wa kijiji hicho kwa uzalishaji mkubwa na kukubali kuuza mbaazi zao kwa mfumo wa stakabadhi ghalani.

Alisema,msimu uliopita bei ya mbaazi katika mnada wa kwanza bei ya chini ilikuwa Sh.850 na bei ya juu Sh.950 na hata katika mnada wa mwisho bei ilikuwa Sh.1,020 tofauti na mwaka huu ambapo bei katika mnada wa kwanza ni Sh.2,016.

Alisema,zao la mbaazi limeendelea kufanya vizuri kutokana na kununuliwa kwa bei kubwa na hivyo kuwa miongoni mwa mazao yanayowaingia wakulima fedha nyingi katika wilaya ya Tunduru.

Hata hivyo,amewataka wakulima kuongeza uzalishaji kwa kupanua mashamba yao na kulima mazao mbalimbali ikiwemo ufuta,korosho na mbaazi ili waweze kupata fedha nyingi na kuondokana na umaskini kupitia shughuli zao za kilimo.

Meneja wa Chama kikuu cha Ushirika(Tamcu Ltd) Imani Kalembo, amewaomba wanunuzi kuongeza bei ya kununua mbaazi ili kuwahamasisha wakulima kuzalisha kwa wingi mbaazi na mazao mengine ya biashara yanayostawi vizuri katika maeneo mbalimbali wilayani humo.

“wanunuzi wakiongeza bei,wakulima wanapata moyo wa kuongeza uzalishaji na kuamini kuwa serikali iko pamoja na wao kwa kusimamia suala la bei ya mazao yao yanayouzwa kupitia mfumo wa stakabadhi ghalani”alisema Kalembo.

Amewaomba wakulima kuwa na utaratibu wa kujitokeza kwa wingi kwenye minada inayofanyika katika maeneo yao, kwani lengo la Chama kikuu ni kuhakikisha minada yote inafanyika kwa uwazi ili wakulima wafahamu bei zinazotolewa na wanunuzi.

Kwa upande wake Afisa ushirika wa wilaya ya Tunduru George Bissan alisema,wakulima wa wilaya hiyo wana bahati kubwa kwa kupata soko la uhakika na bei nzuri ya mazao wanayozalisha.

Bissan amewataka wakulima kuwa na uvumilivu baada ya mavuno ili kuuza mazao kupitia vyama vyao vya msingi vya ushirika kupitia mfumo wa stakabadhi ghalani wenye faida kubwa na kukataa kuuza kwa walanguzi kwa bei ndogo isiyolingana na gharama za uzalishaji.

Amewaonya viongozi wa vyama vya msingi(Amcos),kuepuka udanganyifu badala yake kuwa waaminifu na waadilifu kwa kulipa fedha za wakulima kwa wakati ili kusitokee malalamiko na kushusha hali ya uzalishaji mashambani.

Katika hatua nyingine Bissan,amewahimiza vijana wilayani humo kujikita katika shughuli za kilimo badala ya kutumia muda mwingi vijiweni kucheza pool na bao,tabia inayo warudisha nyuma na kukithiri kwa umaskini miongoni mwao.

Mwakilishi wa wakulima wa mbaazi Seif Kaunda,ameishukuru serikali kwa kusimamia ununuzi wa zao la mbaazi kupitia mfumo wa stakabadhi ghalani kwani umewasaidia kupata soko la uhakika na bei nzuri ambayo inakwenda kuboresha maisha yao na kuhamasisha watu wengi kujikita kwenye kilimo.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live