Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

‘Wakulima hawatakatwa pesa mbegu za pamba’

B26e8a3c1f34b1d35982ef2423ce6f8e ‘Wakulima hawatakatwa pesa mbegu za pamba’

Tue, 19 Jan 2021 Chanzo: habarileo.co.tz

NAIBU Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe, amesema katika msimu wa zao la pamba mwaka huu 2020/21, hakuna mkulima yeyote atakayekatwa pesa za mbegu na viuatilifu.

Alitoa kauli hiyo jana katika kikao cha wadau wa pamba nchini kilichofanyika mjini Bariadi katika Mkoa wa Simiyu.

Alisema katika msimu huu wa 2020/21 hakuna mkulima atakayekatwa pesa kwa ajili ya mbegu na viuatilifu.

Alisema wakulima waliokopeshwa mbegu na ambao watakopeshwa viuatilifu, hawatakatwa wakati wa kuuza pamba yao kama ambavyo imezoeleka kwani serikali itatumia utaratibu mwingine bila kumuumiza mkulima.

"Huko nyuma wakulima walikuwa wanakopeshwa mbegu na viuatilifu kama ambavyo tumefanya mwaka huu, lakini walikuwa wakikatwa wanapoleta pamba yao kuuza, mwaka huu hakuna mkulima atayekatwa," alisema.

Akaongeza: "Serikali katika mkokotoo wa bei ya pamba, ndiko tutaweka hizo gharama za mbegu na viuatilifu ambavyo wakulima mwaka huu wamepewa bure, lakini bei ya mkulima itabaki palepale na hatutamuumiza mkulima tena," alisema Bashe.

Kwa mujibu wa naibu waziri huyo wa kilimo, katika msimu huu wa pamba, hakutakuwepo changamoto ya ukosefu wa viuatilifu na ukosefu wa mbegu kwenda kwa wakulima kwa kuwa maandalizi yamefanyika mapema.

Katika hatua nyingine, naibu waziri huyo alisema katika msimu huu utaratibu wa wakulima wa zao hilo kulipwa kwa njia ya simu au benki na kwamba, hakuna mtu yeyote atakayelipwa pesa taslimu.

"Mfumo huu ulisitishwa kidogo, lakini mwaka huu hakuna mkulima atakayelipwa pesa taslimu; wakulima wote watalipwa kwa njia ya benki au kupitia mitandao mbalimbali ya simu zao,"alisema.

Mkurugenzi wa Bodi ya Pamba, Marko Mtunga, alisema bado kuna changamoto ya tija ndogo katika zao hilo kutokana na baadhi ya wakulima kutofuata kanuni bora za kilimo na kutokuwepo kwa huduma bora za kutosha za ugani.

Mtunga alisema endapo halmashauri zitaimarisha huduma za ugani kwa zao hilo, uzalishaji wa pamba utaongezeka na hakutakuwapo malalamiko kuhusu bei kwa wakulima.

Akifungua mkutano huo, Mkuu wa Mkoa wa Mara, Adam Malima alisema tija katika zao pamba bado ni ndogo, hali inayosababisha uzalishaji kushuka mara kwa mara.

Chanzo: habarileo.co.tz