Waziri wa Ujenzi, Innocent Bashungwa ameiomba Benki ya Dunia kupitia upya masharti ya manunuzi katika mikataba ya utekelezaji wa miradi ya miundombinu ili kutoa fursa kwa wakandarasi wazawa kushiriki katika utekelezaji wa miradi hiyo.
Bashungwa ametoa ombi hilo katika kikao na Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Dunia nchini, Nathan Belete na ujumbe alioambatana nao kujadili mambo mbalimbali yanayohusu sekta ya Ujenzi, leo jijini Dar es salaam.
Bashungwa ameeleza kuwa masharti yanayowekwa katika utekelezaji wa miradi mbalimbali inayosimamiwa na kufadhiliwa na Benki ya Dunia yamekuwa yakiwabana Wakandarasi wazawa na kushindwa kushiriki kwa kutokidhi vigezo katika manunuzi.