Dar es Salaam. Wafanyakazi wa benki nchini wameanza kupewa mafunzo maalumu ya namna ya kutoa msaada hasa wa ushauri kwa Watanzania wanaohitaji mikopo ya nyumba.
Mafunzo hayo yanatolewa kwa ushirikiano baina ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Chuo cha Wafanyakazi wa Benki (BIT) na taasisi inayojihusisha na mikopo ya nyumba ya TMRC.
Mafunzo hayo yatawasaidia watumishi wa benki kuwashauri wateja kukopa nyumba na kuwa na uwezo wa kurejesha kwa wakati.
Akifungua mkutano wa makubaliano ya utoaji wa mafunzo hayo leo Alhamisi Agosti 2, 2018, mkurugenzi wa masoko ya fedha wa BoT, Alexender Mwindamile amesema mkakati wa Serikali ni kuhakikisha masilahi ya wakopaji na wakopeshaji yanalindwa.
“Hizi ni juhudi za kuwasaidia Watanzania wapate makazi bora. Mfumo wa mikopo ya nyumba una faida nyingi kiuchumi. Kwa hiyo tumeona kuna kila sababu ya kutoa elimu kwa wafanyakazi wa benki wawe na uwezo wa kutoa ushauri mzuri,”amesema.