Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega amesema wizara yake ipo mbioni kuanzisha programu ya "BBT" kwa upande wa tasnia ya maziwa ambapo tayari ameshaielekeza Bodi ya Maziwa nchini na kurugenzi ya uzalishaji na masoko kushirikiana na washirika wa maendeleo wa sekta ya Mifugo na Taasisi za fedha ili kuanza utekelezaji wa programu hiyo katika mikoa ya Kagera na Mbeya ambako kuna kiasi kikubwa cha maziwa.
Waziri Ulega alibainisha hayo jana Juni 1, 2023 wakati wa kilele cha maadhimisho ya Kitaifa ya Wiki ya Unywaji Maziwa Duniani yaliyofanyika kwenye Viwanja vya Chipukizi mkoani Tabora.
Alisema kuwa Wizara yake ipo tayari kuanzisha programu hiyo katika Mikoa ya Mbeya na Kagera kwa sababu mikoa hiyo inazalisha maziwa kwa wingi hivyo anaamini itakuwa rahisi kupata matokeo kwa haraka mara baada ya kuifungamanisha rasilimali hiyo katika mnyororo wa thamani.