MKUU wa Mkoa wa Kagera, Fatma Mwassa amewataka wafanyabiashara kuwajibika kulipa kodi kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ili kufanya mabadiliko ya kiuchumi na maendeleo makubwa zaidi mkoani Kagera.
Akizungumza katika ufunguzi wa kampeni ya Tuwajibike inayoendeshwa na mamlaka hiyo, yenye lengo kukuza maendeleo haraka kupitia kodi, RC Mwassa alisema wafanyabiashara wanapaswa kutumia mashine ya risiti za kielekroniki pale mteja anaponunua bidhaa madukani.
Aidha RC Mwassa alisema angependa takwimu za wafanyabiashara wanaotumia mashine za EFD ziongezeke zaidi hivyo ametoa wito kwa TRA mkoani Kagera kuhakikisha wanapita katika maduka ya wafanyabiashara wakubwa na wafanyabiashara wa kati kuhakikisha wanakuwa na mashine hizo.
Alisema Mkoa wa Kagera unapoteza mapato mengi kwa sababu biashara nyingi zinazofanyika hazijarasimishwa hivyo wafanyabiashara wengi wanapanga bidhaaa bila kujali wingi wa mitaji yao kuliko walioko madukani hivyo TRA inapata ugumu wa kukusanya kodi.