Dodoma. Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) imeahidi kushirikiana na Serikali ya Tanzania kukuza uchumi wa wananchi sambamba na kusaidia kufanikisha ujenzi wa miradi mikubwa inayoendelea kujengwa nchini.
Mkurugenzi wa Idara ya Hazina na Masoko wa NBC, Peter Nalitolela amesema hayo leo wakati akizungumza katika kongamano la wadau juu ya upatikaji wa fedha na usimamizi wa hatari zinazoweza kujitokeza katika miamala ya kifedha lililoandaliwa kwa wadau mkoani Dodoma.
Amesema benki hiyo imejizatiti kushirikiana na Serikali pamoja na taasisi zake kuhakikisha nchi inafaidika na kiasi cha pesa inachotumia katika miradi mikubwa ya maendeleo inayoendelea kufanyika.
Amesema kongamano hilo linalohudhuriwa na wadau kutoka Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Tanesco, TPDC na Wizara ya Fedha na Mipango, lina lengo la kuangalia vyanzo mbalimbali vya fedha vinavyopatikana katika miradi mbalimbali mikubwa inayofanywa nchini.
Pia, linalenga kuangalia usimamizi wa hatari katika miamala ya kifedha inayoweza kutokea katika utekelezaji wa miradi hiyo.
Baadhi ya miradi mikubwa inayofanywa nchini ni pamoja na Ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR), mradi wa Umeme wa Mto Rufiji wa Stiegler’s Gorge na ujenzi wa barabara na madaraja.
Pia Soma
- Mbunge hamasa ya uwekezaji wa Uingereza ziarani nchini
- Heche akwamisha kesi ya vigogo Chadema
- Rafiki wa Boby Wine afariki baada ya kutekwa
- Mauaji yanayoendelea Marekani, Rihanna amjibu Rais Trump
“Kikubwa ni kwa NBC kuangalia uwezo wetu kwa njia tofauti tofauti ikiwemo katika kukopesha, lakini pia kuona serikali haipati hasara kutokana na masuala ya riba, fedha za kigeni na kushuka kwa thamani ya shilingi, kwa uwezo wetu tunaweza kushirikiana zaidi na zaidi.”
Mkurugenzi huyo amesema kama inavyofahamika kuwa NBC inamilikiwa kwa pamoja na Serikali ya Tanzania, Benki ya Absa ya Afrika Kusini pamoja na Benki ya Dunia, hii huiweka NBC katika nafasi nzuri ya kusaidia juhudi za serikali.
Katika kongamano hilo pia NBC imeleta wataalam kutoka benki mama ya Absa ili kuweza kuonyesha uzoefu wao walioupata kupitia miamala waliyofanya na serikali za nchi mbalimbali barani Afrika.