Dodoma. Kamati ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji (PIC), imetoa maagizo sita kwa Shirika la Maendeleo la Petroli (TPDC) likiwamo la kupeleka mkataba tata kati ya shirika hilo na Kampuni ya AG & Pgas Limited a/k/a Artumas Group &Partners (Gas) Limited.
Maagizo mengine kwa shirika hilo ni kuhakikisha miradi iliyoanzishwa
na inayoendelea inafanyika kwa ufanisi zaidi, uwekezaji wa bomba la
gesi uendane na mahitaji ya nchi, pamoja na kupunguza gharama za uendeshaji.
Mengine ni kuweka mkakati wa kulipa na kukusanya madeni na kuongeza kasi ya usambazaji wa gesi kwa watumiaji.
Akizungumza leo badaa ya kamati hiyo kukutana na TPDC, Mwenyekiti wa kamati hiyo, Dk Raphael Chegeni amesema sheria iliyopitishwa mwaka
jana na bunge, imetoa fursa kwa mikataba kupatikana kwa urahisi.
“Spika ametoa maagizo kwa kamati hii tupitie mikataba ambayo
baadhi ya mashirika na taasisi zimeingia na wadau kama ina tija kwa nchi. Kwa hiyo tumetoa maagizo mkataba uliopo sasa wa
TPDC na wadau mbalimbali uletwe ili tuusome ili sasa tuone kama utaleta tija zaidi kwa taifa,”amesema Dk Chegeni.
Amesema shirika hilo linakabiliwa na changamoto nyingi ikiwa ya madeni. Imeelezwa kuwa TPDC inadaiwa kushindwa kulipa madeni yake kwa wakati, hali inayosababisha washindwe kutimiza majukumu yake kikamilifu.
“Moja ya wadaiwa wakubwa wakuu ni Tanesco (Shirika la Umeme Nchini)
ambao wanadaiwa Sh 580 bilioni ni fedha nyingi sana,”amesema Dk
Chegeni.
Amesema wameangalia pia matumizi ya gesi kutokana na kamati kuamini kuwa ili iweze kutumika kwa wingi ni lazima ipatikane kwa gharama nafuu.
Amesema suala lingine ni uwezo wa ulipaji wa madeni ambayo TPDC inadaiwa na Benki ya TIB, Sh 64.5 bilioni.
Fedha hizo zilichukuliwa na TPDC na kutumika kama dhamana kwa mkopo wa Sh 2.6 trilioni kutoka Benki ya Exim ya China kwaajili ya ujenzi wa mradi wa bomba la gesi.
Dk Chegeni amesema kamati yake imetoa maelekezo kwa TPDC ipunguze gharama za uendeleshaji zisizo za lazima baada ya kubaini kuna matumizi yasiyoendana na mapato.
Dk Chegeni amesema kamati imeagiza deni la Sh2.6 trilioni lililokopwa na Serikali
kwa ajili ya uwekezaji wa bomba za gesi, lilipwe na Serikali
kuu badala ya kulibebesha mzigo shirika hilo.
Kaimu Mtendaji wa TPDC, Kapulya Musomba amesema licha ya kuwa shirika hilo wanadai kiwango kikubwa cha fedha Tanesco, lakini bado wanaolionea huruma.
Amesema kama watachukua hatua ya kuliondoa katika sekta ya gesi, watakuwa wanaliua kabisa kutoka na uhitaji mkubwa wa gesi unaotakiwa na shirika hilo.
“Wateja wengine ni wale wanaonunua gesi kiwango kidogo, kwa hiyo
ni wajibu wetu sote kushirikiana na Serikali ili kuona Tanesco
inasaidiwa,”amesema.
Hata hivyo, amesema tayari wameshakutana na uongozi wa
Tanesco na wamepanga mkakati wa namna ya kulilipa deni hilo.
Mwakilishi wa Wizara ya Nishati na Madini, Joyce Kisamo
amesema mradi wa
bomba la gesi utaweza kuliingizia taifa mapato kama suala la kutazama faida kwanza litazingatiwa.
Amesema Tanzania haiwezi kuwavutia wawekezaji kwa uwekezaji wao kama utawafanya wapate faida kubwa kuliko nchi.
“Kwasababu utamvutia mwekezaji kwa kuweka incentive (vivutio ) vingi
tu unampa na gesi kwa bei ndogo lakini wewe ndiye unafidia. Mradi wa
bomba la gesi utalipa kama hatutakuwa tumempa mwekezaji kiwango kikubwa (faida) kuliko sisi,” amesema.