Dar es Salaam. Mkurugenzi mkuu wa kampuni ya Lindam Group, Zuhura Muro amesema ili kufikia uchumi wa viwanda ni vyema kuvifufua vyuo vya ufundi na kuwajengea uwezo vijana kutumia rasilimali zilizopo nchini.
Hayo ameyasema leo usiku Oktoba 4, 2018 akichangia mjadala katika Jukwaa la Fikra la Mwananchi linalolenga kujadili fursa, changamoto na ufumbuzi kuelekea uchumi wa viwanda ambalo limeandaliwa na Kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL) na kurushwa moja kwa moja na kituo cha televisheni cha ITV.
Muro amebainisha kuwa bila kufanya hivyo ni vigumu kufikia uchumi wa viwanda na nchi itakuwa inatengeneza watu wanaosubiri kuajiriwa tu.
"Tanzania hatujaweza kutumia rasilimali zetu na hilo ni kutokana na kushindwa kupika watu wenye ujuzi," amesema Muro.
Amebainisha kuwa vyuo vingi vilivyokuwa vikipika vijana hivi sasa vimepandishwa hadhi ya kuwa vyuo vikuu.
"Ifike mahali tutengeneze viwanda kwa kutumia rasilimali zinazotuzunguka hususan kwenye kilimo ambacho ndicho kitenga uchumi cha Watanzania wengi, ufugaji nyuki, mifugo na uvuvi," amesema Muro na kuongeza:
"Tuna maji mengi ambayo hatujayatumia vizuri kwani mpaka sasa katika bahari ya Hindi tuna kilomita 200 za maji ambazo tungeweza kuzitumia kuanzisha viwanda.”