Misungwi. Vyama vya ushirika Wilaya ya Misungwi mkoani Mwanza vimetumia takribani Sh3 milioni za wakulima kusafirisha pamba .
Hayo yamelezwa leo Jumamosi Septemba 28, 2019 na viongozi wa vyama hivyo mbele ya naibu Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe.
Wamesema walilazimika kutumia fedha hizo kwakuwa hawakupata fedha zinazotolewa na mnunuzi wa pamba ambazo ni asilimia 33 za ushuru.
Mhasibu wa Chama cha Ushirika (Amcos) cha Mwaniko, Amos Luhega amesema alilazimika kutumia fedha za wakulima Sh1 milioni kwa ajili ya kusafirisha kilo 59,360 za pamba kwa kuwa chama hicho hakikuwa na fedha kwa sababu hakikulipwa kampuni zinazonunua pamba.
Mhasibu wa Amcos ya Ibongoya, Elizabeth Zephania amesema ametumia Sh100,000 za wakulima kwa ajili ya kukarabati ghala lililotumika kuhifadhia pamba.
Kwa mujibu wa mkuu wa Wilaya ya Misungwi, Juma Sweda amesema kaya 15,000 zinalima pamba wilayani humo.
Pia Soma
- Siri ya wakazi Iringa kuchangamkia matunda pori
- DC Temeke ataka siku moja zaidi tamasha la Jamafest
- VIDEO: Majaliwa amkalia kooni mkurugenzi manispaa Iringa ujenzi wa ukumbi eneo la shule
Kwa upande wake Bashe amezitaka kampuni za ununuzi wa pamba kufanya malipo ya awali kwa vyama vya msingi vya ushirika ili navyo viwalipe wakulima fedha zilizotumika kusafirisha pamba.
Taarifa ya mkurugenzi mkuu wa Bodi ya Pamba (TCB), Marco Mtunga kwa wajumbe wa mkutano wa 16 wa wadau wa zao hilo uliofanyika jijini Mwanza Septemba 27, 2019, kiasi cha Sh150 bilioni zinadaiwa na wakulima wa pamba msimu wa mwaka 2018/19 na zaidi ya Sh240 bilioni zimelipwa kwa wakulima kupitia vyama vya ushirika.