Dodoma . Wizara ya Kilimo nchini Tanzania imesema iko mbioni kuvifuta vyama vya ushirika 3,436 kati ya vyama 11149 vilivyoandikishwa na kudaiwa kuwa ni mfu.
Vyama hivyo vinadaiwa havijulikani vilipo, viongozi wake hawajulikani waliopo, kukosekana kwa taarifa zake, kutofunga mahesabu ya kila mwaka, bodi kutokukutana pamoja na kutofanya mikutano mikuu ya kila mwaka.
Waziri wa Kilimo, Japhet Hasunga amesema hayo jijini Dodoma wakati akizungumza na waandishi wa habari leo Jumapili Januari 5, 2020.
Amesema kati ya vyama hivyo, 1,250 vinasuasua na vyama hai ni 6,463.
“Tunakusudia kuvifuta vyama 3,436 ambavyo ni mfu, lakini tutatoa tangazo kwenye gazeti la Serikali likionyesha idadi ya vyama hivyo, pia tutatoa muda wa siku 90 ili mtu ambaye ataona chama chake hakistahili kufutwa ajitokeze,” amesema Hasunga.
Wakati huo huo, Waziri huyo ametangaza mbegu mpya za mazao 40 zinazoamza kutumika mwaka 2019/20.
Hata hivyo amesema mahitaji ya Mbegu Tanzania ni tani 186,000 na uzalishaji wa Mbegu hizo kwa Tanzania hata nusu haijafika.