Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Vodacom sasa kuanza kutumia miundombinu ya serikali

TTCL Plc Mkurugenzi Mkuu wa TTCL akizungumza wakati wa hafla ya utiliaji saini

Wed, 20 Apr 2022 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Vodacom Tanzania imesaini mkataba na Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano (NICTBB) wenye thamani ya Dola za Kimarekani milioni 4.59 (sawa na Shilingi Bilioni 10.6 za Kitanzania), utakaoiwezesha kampuni hiyo kutumia miundombinu ya mkongo inayomilikiwa na serikali ili kuongeza mawasiliano vijijini katika hafla iliyofanyika leo Makao Makuu ya TTCL jijini Dar es Salaam.

Uwekezaji huu unakuja baada ya uwekezaji wa awali wa Dola za Marekani 6,223,500(sawa na Shilingi Bilioni 14.5 za Kitanzania) uliofanyika mwezi Oktoba 2021 na unatazamiwa kupeleka mtandao wa kasi katika maeneo ya vijijini ili kufikia maeneo mengi zaidi ya nchi ambayo bado hayajahudumiwa. Kwa kuongeza ufikiaji wa mtandao katika maeneo ya pembezoni ya nchi, wananchi wengi zaidi wataweza kufikia vifaa vya kidijitali, kama vile huduma za afya, utoaji wa elimu na kupata habari za kilimo na pia kuendeleza ukuaji wa ujumuishaji wa huduma za kifedha kitaifa.

Mkataba huo ulisainiwa kati ya Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL Corporation), Mhandisi Peter Rudolph Ulanga na Mkurugenzi Mkuu wa Vodacom Sitholizwe Mdlalose unalenga kuboresha mawasiliano ya simu na data za Vodacom katika mikoa ya kanda ya ziwa, kati na kusini mwa Tanzania katika harakati za kuibadilisha nchi kuwa ya watu wenye maarifa kupitia matumizi ya TEHAMA (ICT).

Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dkt Jim Yonaz ambaye alishuhudia utiaji saini mkataba huo alisema “Dira ya Serikali ni kukuza TEHAMA (ICT) ambapo serikali inatekeleza mkakati wa kuhakikisha asilimia 80 ya wananchi wanaunganishwa kidijitali ifikapo 2025. Upanuzi wa Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano utatufikisha karibu na lengo hili. Tumejitolea katika hili kwa sababu tunataka kuhakikisha Watanzania wote wanapata fursa ya kufurahia manufaa ya kuunganishwa kidijitali. Tunatambua jukumu muhimu la makampuni ya simu za mkononi katika kuifikia jamii. Tunaishukuru Vodacom Tanzania na ushirikiano wake katika kutumia rasilmali hii ambayo nchi imewekeza na kuwezesha kuwafikia Watanzania”.

Akizungumza wakati wa hafla ya utiaji saini huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom Tanzania Sitholizwe Mdlalose alisema, “Vodacom Tanzania inalenga kubadilisha nchi kuwa ya watu wenye maarifa kupitia matumizi ya TEHAMA huku tukipunguza mtawanyiko wa kidijitali pamoja na kuimarisha uwezo wa kiushindani wa watoa huduma ya data na sauti nchini. Ushirikiano huu unakuja ili kusisitiza dhamira yetu kama kampuni katika kukabiliana na ongezeko la mahitaji ya huduma za kidijitali nchini.”

Vodacom Tanzania PLC imekuwa mdau mkuu wa matumizi ya miundombinu ya NICTBB tangu mwaka 2012, mkataba wa kukodisha wenye thamani zaidi ya dola za Kimarekani milioni 50 uliosainiwa tangu mwaka 2012. Katika kipindi cha miaka mitano TTCL ambao wanasimamia NICTBB imefanya kazi na kampuni ya mawasiliano nchini kwa matumizi hayo ya miundombinu ya mkongo kama mdau mkuu katika matumizi ya NICTBB.

Akifafanua kuhusu utoaji wa huduma kwenye Mkongo wa Taifa, Sitholizwe aliendelea kusema, “Kama kampuni ya huduma za teknolojia, Vodacom Tanzania inategemea mtandao wa kasi ili kufikisha huduma muhimu za kijamii na kibiashara nchini. Tumeanzisha huduma za kifedha kwa kutumia jukwaa letu la M-Pesa, tuko mstari wa mbele katika kutoa maudhui ya elimu kwenye tovuti yetu ya E-Fahamu pamoja na programu yetu iliyozinduliwa hivi majuzi ya m-mama ambayo inafanya kazi ya kupunguza vifo vya uzazi na watoto nchini. Vodacom pia imeanza kushirikiana na wizara mbalimbali pamoja na taasisi za serikali, kama vile TRA, TARURA, TANESCO na Mamlaka za Maji za Mikoa mbalimabli ili kufikisha huduma za kidijitali kwa taifa. Tunafurahia sana kuwa na kituo hiki cha kutuwezesha kusambaza huduma hizi kwa manufaa ya Watanzania wengi zaidi.”

Mhandisi Peter Rudolph Ulanga, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL Corporation) anayesimamia NICTBB kwa niaba ya Serikali alisema, “Tunafurahi kuona waendeshaji wengi wanatumia NICTBB kwani miundombinu ilitengenezwa kwa lengo kuu la kusaidia nchi kutambua agenda ya TEHAMA. Ninaamini miundombinu iliyokodishwa kwa Vodacom itaimarisha matumizi ya TEHAMA kwa maendeleo endelevu ya kijamii na kiuchumi ikiwa ni pamoja na utekelezaji wa huduma za kielektroniki za serikali, elimu ya kidijitali, afya ya kielektroniki, biashara ya kielektroniki na mengine mengi ndani na nje ya nchi”.

Mhandisi Ulanga aliendelea kueleza dhamira yake ya kutanguliza ubora wa huduma, “Kama watoa huduma, tutahakikisha tunatoa rasilmali bora kwa wadau wote wa mawasiliano nchini.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live