Dar es Salaam. Bodi ya wakurugenzi ya kampuni ya Vodacom Tanzania imemteua mwenyekiti wa mpito, Margaret Ikongo kuanzia Desemba Mosi, 2019 akichukua nafasi iliyoachwa wazi na marehemu Ali Mufuruki aliyetangaza kujiuzulu.
Taarifa iliyotolewa leo Jumatatu Desemba 16, 2019 na katibu wa kampuni hiyo, Caroline Mduma imeeleza kabla ya uteuzi huo Margaret alikuwa mjumbe na mwenyekiti wa kamati ya ukaguzi, dharura na utekelezaji tangu Novemba 2017.
“Katika kipindi hiki cha mpito, Margaret atashirika nafasi hiyo na kuachia uenyekiti wa kamati ya ukaguzi, dharura na utekelezaji hadi mchakato wa kumpata mwenyekiti mpya wa bodi utakapokamilika,” imeeleza taarifa hiyo
Oktoba 18, 2019 Ali Mufuruki alitangaza kujizulu akisema anataka muda wa ziada wa kuendelea na biashara zake.
Mufuruki ambaye ni Mwenyekiti na Ofisa Mtendaji mkuu wa kampuni ya Infotech investment Group alishika wadhifa huo kuanzia Agosti 1, 2017.
Hata hivyo, Desemba 8, 2019 Mufuruki anayetajwa kuwa miongoni mwa mabilionea wa Kitanzania alifariki dunia akiwa nchini Afrika Kusini na mwili wake ulizikwa Desemba 10, 2019 katika makaburi ya Kisutu jijini Dar es Salaam.