Dar es Salaam. Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi,Vijana na Ajira, Anthony Mavunde amekipiga faini ya Sh9.5 milioni kiwanda cha Azania na kiwanda cha Salifrica Sh5 milioni kwa kukiuka sheria ya usalama na afya mahali pa kazi
Viwanda hivyo pia vimekutwa na kosa la kutowapatia wafanyakazi vifaa kinga kwa ajili ya kulinda usalama wao wanapokuwa kazini.
Mavunde amechukua uamuzi huo leo alipotembelea viwanda hivyo vilivyopo wilayani Temeke jijini Dar es Salaam.
Sanjari na faini hiyo Mavunde ametoa maelekezo kwa uongozi wa viwanda hivyo kutoa mikataba kwa wafanyakazi wao kwa mujibu wa sheria ya ajira na mahusiano Kazini Na. 6/2004.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, wafanyakazi wa viwanda hivyo wameishukuru Serikali kwa kutatua changamoto zao za miaka mingi za ukosefu wa mikataba ya kazi na hivyo kukosa haki zao za kimsingi.