Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Viwanda kupata korosho za uhakika 2020/2021

32200ac45825ac42e7fa39905a596aaf Viwanda kupata korosho za uhakika 2020/2021

Wed, 23 Sep 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

SERIKALI imepanga kuweka utaratibu mahsusi wa viwanda vya kubangua korosho nchini ili kuwa na uhakika wa malighafi katika msimu ujao wa ununuzi wa korosho ghafi, amesema Naibu Waziri wa Kilimo, Omary Mgumba.

Akizungumza katika ufunguzi wa kikao kazi cha kujadili mkakati wa kuviwezesha viwanda vya kubangua korosho ndani ya nchi kupata malighafi ya kutosha kilichofanyika mjini Mtwara, Mgumba alitaka kikao hicho kujadili namna ya kuhakikisha korosho ya wakulima inapata soko la uhakika.

“Tumekutana hapa kama serikali kujadili namna tutakavyowezesha viwanda vyetu 40 vya kubangua korosho ndani ya nchi kupata malighafi ya kutosha msimu huu 2020/2021,” alisema.

Mgumba alisema kuna viwanda 40 vya kubangua korosho nchini vyenye uwezo wa awali wa kubangua tani 170,476 kwa mwaka, lakini uwezo wa sasa ni kubangua tani 59,776 za korosho.

Mgumba alisema kikao hicho ni sehemu ya utekelezaji wa maagizo ya Rais John Magufuli kuhakikisha nchi inauza nje korosho iliyoongezwa thamani ili kuwafanya wakulima wapate tija na nchi kupata fedha za kigeni.

Uzalishaji korosho ghafi kufikia mwaka 2025 umepangwa kuongezeka kutoka tani 313,826 mwaka 2017/2018 hadi tani 1,000,000 ifikapo mwaka 2025.

Ilibainika pia kuwa, Wizara ya Kilimo kupitia vituo vyake 17 vya utafiti wa kilimo (Tari), ndiyo inayoratibu upatikanaji wa mbegu bora za korosho.

Akizungumza kwa niaba ya wakuu wa mikoa inayolima korosho nchini, Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Christina Mndeme alisema Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya Mwaka 2020 inasisitiza zao la korosho kuongezwa thamani nchini ili lisaidie wakulima kupata uhakika wa soko na kuzalisha ajira katika viwanda.

Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Gelasius Byakanwa alisema nchi inahitaji viwanda vingi vya kubangua korosho ili wakulima wawe na uhakika wa soko.

Naye Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Gerald Kusaya alisema wizara yake ipo katika mkakati wa kuwafundisha maofisa ugani katika halmashauri zote zinazolima korosho katika mikoa 17 kanuni bora za uzalishaji korosho ili kuongeza tija na kusaidia wakulima kuzalisha kwa ubora.

Chanzo: habarileo.co.tz