Serikali imewaita wawekezaji kutoka sekta binafsi wawekeze katika viwanda 20 vilivyobinafsishwa na sasa vimerudishwa serikalini.
Viwanda hivyo ni kati ya viwanda 156 vilivyobinafsishwa kwa mujibu wa sera iliyotekelezwa miaka ya 1990 nchini. Viwanda 68 havikujiendesha kwa mujibu wa mikataba na 88 vilifanya vizuri.
Waziri wa Viwanda na Biashara, Profesa Kitila Mkumbo jana alisema kati ya viwanda hivyo 68
ambavyo havikufanya kazi vizuri, 48 wawekezaji hawakuzingatia matakwa ya mikataba na 20 kati ya hivyo tayari vimerejeshwa serikalini.
“Baadhi ya viwanda vilikosa sifa ya kuwa viwanda baada ya kubinafsishwa miaka ya 1990. Timu ya serikali iliundwa na ikaingia katika mazungumzo na wawekezaji na kukubaliana kurudisha kisheria viwanda hivyo serikalini. Tayari viwanda 20 vimerejeshwa serikalini havina migogoro vipo mikononi mwa serikali,” alisema Profesa Mkumbo.