Mamlaka ya udhibiti wa huduma za Nishati na maji EWURA,imeanza mchakato wa kuhamasisha vituo vyote vya mafuta zaidi ya 1,000 nchini kujenga miundombinu asilia
Imesema lengo ni kuokoa gharama za matumizi kwa wamiliki wa vituo na vyombo vya usafiri.
Hayo yalisemwa mwishoni mwa wiki na Meneja Mawasiliano na Uhusiano EWURA, Titus Kaguo, wakati wa semina kwa waandishi wa habari wa mikoa ya Nyanda za Juu Kusini ya Mbeya, Rukwa, Songwe, Katavi, Njombe na Ruvuma.
Alisema serikali imejipanga kuhamasisha matumizi ya gesi asilia inayochimbwa Mtwara na Songosongo ambapo gesi inatumika kwenye viwanda, na kwamba jumla ya nyumba 300 za mkoani Mtwara zimeunganishwa na gesi hiyo.
Kitu ambacho serikali inakifanya kwa sasa ni kuhamasisha matumizi ya gesi kwenye magari na vituo vya mafuta kwa sasa, kuna vituo viwili ambapo kimoja tayari kinatoa huduma za gesi asilia,” alisema Kaguo.
Aliongeza kuwa hadi sasa jumla ya magari 300 yameunganishwa na mfumo wa gesi asilia na kwamba lengo ni kuhakikisha magari yote yanaunganishwa kwenye mfumo huo ili kupunguza gharama uendeshaji na kuhimiza matumizi ya nishati mbadala.
Mmoja wa wanahabari, Emmanuel Lengwa, aliiomba EWURA kusimamia bei elekezi za mafuta kwa maelezo kuwa kumekuwa na udanganyifu kwenye vituo vya mafuta.
Alisema kuna udanganyifu unaofanyika kwenye vituo vya mafuta kwa sababu fedha anayotoa mteja ni tofauti na kiasi cha mafuta kinachopatikana.
Meneja wa Mamlaka hiyo Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini, Karim Ally, aliwaomba wanahabari kutoa ushirikiano kwa mamlaka hiyo ili kuboresha huduma za nishati na maji.
Alisema EWURA wanasimamia taasisi mbalimbali, hivyo aliziomba mamlaka zinazofanya kazi pamoja kuhakikisha wanatoa huduma ipasavyo.