Dar es Salaam. Waziri wa Uwekezaji, Angellah Kairuki amewataka wafanyabiashara wanawake wa Taasisi ya Sekta Binafsi nchini (TPSF) kuisoma hotuba ya bajeti ya Serikali na kubaini fursa zilizomo zitakazowawezesha kufanikisha malengo yao.
Waziri amesema hayo alizungumza na wanawake hao jijini Dar es Salaam na kuwaeleza kuwa Serikali imedhamiria kuboresha mazingira ya kufanya biashara na kulinda uwekezaji.
“Tafuteni wataalamu wawachambulie hotuba ya bajeti muone fursa zilizopo. Bajeti imeondoa kodi na tozo 54, tumieni fursa hiyo kufanya biashara,” alisema Waziri Kairuki.
Amesema Serikali inaadaa muswada wa kuboresha mazingira ya biashara utakaowasilishwa bungeni Novemba na kuwataka wanawake hao kutoa mawazo yao kupitia TPSF ili yapelekwe kwenye kikosikazi cha kupunguza kodi.
Kairuki amesema bajeti ya mwaka 2019/20 imewapa unafuu mkubwa wafanyabiashara hivyo wanapaswa kufahamu yaliyopo ili wazitumie fursa zinazowafaa kulingana na miradi waliyonayo.
Kwa upande wake, mwakilishi wa wanawake wazalishaji wa TPSF, Fatuma Kange amesema wamedhamiria kutengeneza mabilionea 20 kati ya 100 ambao Rais John Magufuli anatamani kuwaacha atakapokuwa anaondoka ikulu.
Pia Soma
- VIDEO: Majeruhi 17 wa ajali ya treni waruhusiwa, watatu hali zao bado
- Polisi Kilimanjaro wanasa ndoo 60 za samaki wachanga
- Kamati ya Bajeti yabadili msimamo ETS
Mwakilishi wa chama cha wafanyabiashara wanawake Mkoa wa Kigoma, Doroth Takwe amesema pasipoti za muda wanazotumia kuvuka mipaka ya nchi zinawagharimu fedha nyingi kwa sababu wanatakiwa kuihuisha kila siku wanapovuka mpaka kuingia nchi nyingine.
Takwe ameiomba Serikali kuwatengenezea vitambulisho maalumu watakavyovitumia kati ya miezi mitatu mpaka sita ili kuwapunguzia usumbufu pia.