Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Uzalishaji umeme kufikia lengo ndani ya miaka 5

E671775371152e784465cdfaf9fb9c93 Umeme

Thu, 16 Jul 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

SERIKALI inatarajia kuongeza uzalishaji wa umeme nchini kufi kia lengo la kuwa na megawati 10,000 ndani ya miaka mitano ijayo. Waziri wa Nishati, Medard Kalemani alisema hayo ni mambo ya kipaumbele ambayo wizara imepanga kuyatekeleza.

Megawati hizo zitafikiwa kwa kutekeleza miradi mikubwa ikiwamo mradi wa kuzalisha umeme katika Mto Rufiji wenye megawati 2,115 na miradi ya kufua umeme kwa kutumia gesi asilia ya Kinyerezi I - Extension wenye megawati 185.

Miradi mingine na megawati kwenye mabano ni mradi wa Mtwara (300), Kakono (87), Malagarasi (45), Kikonge (330), Ruhudji (358) na Lumakali (222) pamoja na miradi ya nishati jadidifu yenye megawati 950.

Serikali inatarajia kuimarisha mifumo ya usafirishaji wa umeme kwa kutekeleza miradi mbalimbali ya usafirishaji umeme ikiwa ni pamoja na mradi wa North - West Grid Extension wa kilovoti 400 (Mbeya – Sumbawanga- Mpanda – Kigoma – Nyakanazi).

Mingine na kilovoti kwenye mabano ni Singida - Arusha - Namanga (400), Rufiji – Chalinze – Kinyerezi na Chalinze – Dodoma (400), Rusumo – Nyakanazi (220), Geita – Nyakanazi (220), Bulyanhulu – Geita (220,) Tabora – Kigoma, Tabora – Mpanda wenye Kilovoti 132.

Alipohutubia Bunge la 11 hivi karibuni, Rais John Magufuli alisema serikali inaendelea kutekeleza miradi mingine kwa kutumia vyanzo vingine ikiwamo maji, gesi asilia, jua na upepo.

Akiwasilisha bungeni makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Nishati kwa mwaka 2020/20, Waziri Kalemani alisema yapo mafanikio makubwa katika sekta ndogo ya mafuta na gesi ikiwapo ongezeko la gesi asilia.

Kalemani katika kipindi cha miaka mitano cha Serikali ya Awamu ya Tano, utekelezaji wa mipango ya maendeleo katika sekta ya nishati umepata mafanikio makubwa ikiwamo kuongezeka kwa gesi asilia iliyogunduliwa kutoka futi za ujazo trilioni 55.27 mwaka 2015 na kufikia futi trilioni 57.54 mwaka huu sawa na ongezeko la futi trilioni 2.27.

Mafanikio mengine ni kuongezeka kwa kasi ya usambazaji wa gesi asilia ambayo kufikia Aprili mwaka huu, katika mikoa ya Dar es Salaam, Pwani na Mtwara, jumla ya nyumba za wateja wa awali zaidi ya 1,000 zimefikishiwa miundombinu ya usambazaji gesi asilia na viwanda 48 vimeunganishwa.

Waziri alisema mafanikio mengine ni kuongezeka kwa ushiriki wa Watanzania katika miradi ya mafuta na gesi asilia.

Hadi Machi mwaka huu, kampuni 457 zimeorodheshwa katika kanzidata iliyoziwezesha kushiriki katika miradi mbalimbali.

Serikali imefanikisha kuendelea kuimarika kwa Mfumo wa Uagizaji wa Mafuta kwa Pamoja (BPS) ambao umeongeza uhakika wa upatikanaji wa mafuta nchini na kupunguza gharama za uagizaji.

Chanzo: habarileo.co.tz