Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Utalii wa meli kuiingizia Tanzania Sh1 trilioni

Thu, 6 Jun 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dodoma. Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk Hamisi Kigwangalla amesema wanawekeza katika maeneo mapya ya utalii ikiwemo utalii wa meli utakaoingiza Taifa pato la zaidi ya Sh1 trilioni kwa mwaka.

Maeneo mengine walioanza mchakato wa kuwekeza ni utalii wa mikutano, fukwe na utamaduni.

Akizungumza katika mahojiano maalum na Mwananchi juzi Jumanne Juni 4, 2019, Dk Kigwangalla amesema kwa mwaka 2019 wamefanikiwa kupata meli za utalii zaidi ya 11 zilizoingia Tanzania.

Amesema utalii wa meli ni eneo litakalosaidia kupata watalii wengi kwa muda mfupi na kwa jitihada za muda mfupi.

“Inakadiriwa kama tukiwekeza Sh150 bilioni tutapata zaidi ya Sh 1trilioni kwenye pato la Taifa katika eneo hili,” amesema.

Amebainisha kuwa tayari wameandika andiko kwa   Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) ili kutenga eneo na wanatarajia kutangaza zabuni Juni 2019 kwa ajili ya  ujenzi wa eneo hilo.

Pia Soma

Amesema zabuni hiyo ni kwa ajili ya ujenzi wa gati maalum kwa ajili ya meli za utalii zitakazokuja nchini na kwamba katika eneo lote kutakuwa na taasisi zinazohusiana na wageni wanaoingia nchini.

Mbunge huyo wa Nzega Vijijini amesema watalii watapata nafasi ya kushuka na kwenda katika vivutio vingine vya utalii kabla ya kurejea katika meli.

“Hii iko katika hatua nzuri. Pia tutajenga utalii wa mikutano, utalii wa fukwe na utamaduni. Eneo limeshapatikana Kigamboni (jijini Dar es Salaam),” amesema.

Waziri huyo amesema tayari mradi umeshaandikwa na wako katika hatua za mwisho za kuupitisha ndani ya Serikali ili waanze kutekeleza.

Chanzo: mwananchi.co.tz